HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, January 6, 2018

WAZIRI MKUU AAGIZA MAAFISA KILIMO WASAMBAZWE

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiangalia mche wa Kahawa, wakati alipotembelea kituo cha utafifti wa zao la kahawa (TACRI) kilichopo kwenye kijiji cha Ugano Wilaya ya Songea, Mkoani Ruvuma, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Ruvuma, kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Kituo hicho, Dkt. Deusdedit Kilambo. Januari 5, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua kitalu cha miche ya Kahawa, wakati alipotembelea kituo cha utafifti wa zao la kahawa (TACRI) kilichopo kwenye kijiji cha Ugano Wilaya ya Songea, Mkoani Ruvuma, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Ruvuma, kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Kituo hicho, Dkt. Deusdedit Kilambo na katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme Januari 5, 2018
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi waliofika kumlaki, wakati alipotembelea kituo cha utafifti wa zao la kahawa (TACRI) kilichopo kwenye kijiji cha Ugano Wilaya ya Songea, Mkoani Ruvuma, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Ruvuma. Januari 5, 2018.
  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiangalia kahawa kwenye mashine ya kusagia kahawa, wakati alipotembelea kiwanda cha kahawa cha Mbinga Coffee kilichopo Mbinga Mjini Wilayani Songea, Mkoani Ruvuma, kushoto ni Meneja Uzalishaji Rabiel Ulomi na kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christina Mndeme. Januari 5, 2018.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiangalia sampuli za kahawa kwenye, wakati alipotembelea kiwanda cha kahawa cha Mbinga Coffee kilichopo Mbinga Mjini Wilayani Songea, Mkoani Ruvuma, kulia ni Meneja Uzalishaji Rabiel. Januari 5, 2018.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiongea na Watumishi wa Halmashauri ya Mbinga, Mkoani Ruvuma, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Ruvuma. Januari 5, 2018.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia mkono wananchi wa Mbinga Mjini, wakati akiwasili kwenye mkutano wa hadhara aliyouitisha kwenye Uwanja wa Michezo Mbinga Mjini Wilayani Songea, Mkoani Ruvuma. Januari 5, 2018.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi wa Mbinga Mjini, kwenye mkutano wa hadhara aliyouitisha kwenye Uwanja wa Michezo Mbinga Mjini Wilayani Songea, Mkoani Ruvuma. Januari 5, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) 
*Ataka takwimu za kahawa ziwe tayari ifikapo Feb. 28

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri za Mji na Wilaya za Mbinga wahakikishe kuwa wanaunda kanda za kilimo na kuwasambaza maafisa kilimo wao badala ya kuwaacha wakae maofisini.

Ametoa agizo hilo jana jioni (Ijumaa, Januari 5, 2018) wakati akizungumza na watumishi na madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga pamoja na Halmashauri ya Mji wa Mbinga, kwenye ukumbi wa Jumba la Maendeleo, mjini Mbinga.

“Mkurugenzi wa TC na DC chuja maafisa kilimo ulionao na uhakikishe wanabakia watatu tu. Abaki DALDO, mtu wa horticulture na mthamini, wengine wote wasambaze kwenye kanda ili wasimamie wakulima wakiwa huko huko. Hili litekelezwe na Mkuu wa Wilaya ulisimamie” alisema.

Aliwataka maafisa kilimo wa zao la kahawa waende vijijini na kufanya sensa ili waweze kubaini wana wakulima wangapi wanaozalisha kahawa. “Afisa kilimo wa wilaya lazima ujue kijiji kina wakulima wangapi wa kahawa, na wana ekari ngapi? Na katika ekari hizo, ana miche mingapi? Hii itaisaidia Serikali ijue inahitaji dawa za aina gani, mbolea kiasi gani na miche mingapi kwa wakulima wake,” alisema.

“Ninataka hizi takwimu ziwe zimekamilika ifikapo tarehe 28 Februari, mwaka huu,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka maafisa ushirika wa wilaya hiyo wakasimamie uundwaji wa AMCOS mpya na kuimarisha zile za zamani ambazo zinafanya kazi vizuri. 

“Maafisa ushirika ninataka nipate takwimu ya AMCOS very strong (ambazo ziko imara) kwenye wilaya yako. Iifikapo tarehe 28 Febriari, takwimu hizi ziwe zimekamilika. Kama kuna AMCOS nzuri ziimarisheni, itisha uchaguzi ili uanze na uongozi mpya,” alisisitiza.

Aliwaeleza watumishi na madiwani kwamba Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kurudisha heshima ya zao hilo ambapo zamani iliweza kusomesha watoto kadhaa kwenda sekondari kutokana na mfuko wa kahawa.


“Zamani zao la kahawa lilikuwa likisomesha watoto wa wakulima, sasa hivi hakuna hata anayefaidika na zao hili. Tunataka zao hili liwanufainishe wakulima, iinue uchumi wa wanaMbinga, isomeshe watoto na iwezeshe wakulima kujenga majumba,” alisema.


Alisema kuanzia msimu ujao wa Mei, Juni na Julai 2018, ununuzi wa kahawa utafanywa na vyama vya msingi vinavyotambulika kwa maafisa ushirika.

Aliwaonya watumishi wa Halmashauri hizo waache kutoa vibali vya ununuzi wa kahawa kwa watu binafsi wanaomiliki kampuni za kununua kahawa. “Halmashauri ndiyo mnatoa vibali vya kampuni kununua kahawa. Huu ni mwisho sasa. Hatuna mnunuzi binafsi wala hatuna kampuni binafsi, hawa wote tukutane kwenye mnada,” alisema.

Alisema hataki kuona watumishi wa Halmashauri wakionesha vibali vya kununua kahawa kama moja ya chanzo cha mapato kwenye Halmashauri hizo. “Ni marufuku kuingiza vibali kwenye mapato ya Halmashauri,” alisema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
JUMAMOSI, JANUARI 6, 2018.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad