HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, December 23, 2017

“VIONGOZI WA DINI WASIKATISHE TAMAA WAUMINI KUKABILI UKIMWI”- DK. MABOKO

VIONGOZI wa madhehebu mbalimbali ya kidini wameombwa kusaidia kuondoa unyanyapaa wa wagonjwa wa Ukimwi ikiwa ni sehemu kamili ya kukabiliana na janga hilo nchini. Aidha wametakiwa kutumia program mbalimbali walizonazo katika mahubiri na kazi zao kuhakikisha kwamba taifa haliwi na maambukizi mapya ya Ukimwi na wale waliokuwa nao wanathaminika.
 Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk. Leonard Maboko katika mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo. Alisema wakati taifa linapata maambukizi mapya 81,000 kwa mwaka, si sahihi kwa viongozi hao wa kidini kuupambanisha ugonjwa huo na mshahara wa dhambi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk. Leonard Maboko akizungumza wakati akifungua mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo.(Picha zote na The Beautytz)
Alisema pamoja na ukweli kuwa mshahara wa dhambi ni mauti, lakini ni kweli pia kwamba wapo ambao wanapata ugonjwa huo bila wao kufanya chochote kile. “Mke yupo nyumbani, mme anachepuka na kuleta ukimwi nyumbani kwa mama… kama tukisema Ukimwi ni dhambi, huyo mama ana dhambi yake nini? Na mtoto aliyezaliwa na Ukimwi, tatizo la mtoto nini?” aliuliza Mkurugenzi akisisitiza haja ya kuondokana na unyanyapaa na kusaidia kwa pamoja kukabiliana na janga hilo. Unapotoa hotuba na kusema kwamba utakufa na Ukimwi wako, haitoi tumaini kwa mgonjwa na wewe unaweza kuwa sababu ya yeye kuamua kuambukiza watu zaidi alisema Mkurugenzi huyo. Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk. Leonard Maboko akizungumza na washiriki wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo.
 “madhehebu yana nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko katika shughuli za Ukimwi” anasema Mkurugenzi na kuongeza kuwa yuko katika mapambano na Ukimwi kwa miaka 22 na ana kila sababu ya kusema kwamba madhehebu ya dini yana mchango mkubwa katika kampeni dhidi ya Ukimwi. Anasema akiwa mchungaji (alitolewa katika kazi hiyo) anaamini ipo haja ya kuwapo na mabadiliko ikiwa mapambano hayo yanatakiwa yafanikiwe. Mwakilishi wa UNESCO katika mkutano huo, Herman Mathias ambaye pia ni Mratibu wa Ukimwi Unesco akifafanua jambo wakati wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo uliofadhiliwa na UNESCO.
Katika mkutano huo ambao umefadhiliwa na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) alisema kwa muda sasa imekuwa ukisimama na kutaja Ukimwi unaonekana kama umetaja dhambi hali ambayo inaongeza unyanyapaa na pia kuwafanya watu wasiwe wa wazi na afya zao. Aidha alisema kwamba kwa sasa kuna tatizo la wanaume wengi kutopima afya zao na hata wakipima hawafuati maelekezo na wanakuwa wa kwanza kufa kutokana na kushindwa kutumia dawa inavyotakiwa. Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mwitikio wa Kitaifa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Audrey Njelekela akizungumza kuhusu nafasi ya viongozi wa dini katika kuleta mabadiliko ya mapambano dhidi ya Ukimwi kwenye mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.

 Alisema kwamba kuwa na nusu ya Watanzania wanaoabudu Mungu kunatoa takwimu zisizo rasmi kwamba watu wengi wanasikiliza mafundisho hivyo wakati umefika kwa wahubiri na viongozi wengine wa dini kutumia madhehebu kufunza maadili na kuepusha maambukizi mapya. Alisema dini zipo kwa ajili ya kuwanusuru wanadamu na dhambi na kwa kuwa imeelezwa hata katika kitabu, kwamba mgonjwa hufuata tabibu, kuendelea kuwasema wenye ugonjwa huo haitasaidia kurekebisha hali bali kuifanya iwe ngumu zaidi. Pamoja na kutaka viongozi hao kupanga namna ya kuwatia moyo waumini wao kutambua hali zao na kuwasaidia katika kutumia dawa kwa ukamilifu, Mkurugenzi huyo alisema hali ya Ukimwi nchini Tanzania kwa sasa ni asilimia 4.7 kutoka asilimia 5.1 miaka minne iliyopita. Mratibu wa shughuli za watoto na vijana TACAIDS, Grace Kessy akieleza kuhusu kutekeleza maazimio ya ESA ya mwaka 2013 ambapo nchi zinahamasishwa kutoa elimu kubwa kwa vijana wao kuhusu afya ya uzazi wakati wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.
Aidha alisema kwamba pamoja na virusi kuonekana kufubazwa kwa asilimia 52 mikoa ya Njombe, Iringa na Mbeya hali ya maambukizi bado ipo juu huku mikoa ya Mtwara, Lindi na Arusha ikiwa chini. Alisema pamoja na kuonekana kwamba kiwango cha maambukizi kimeshuka mtu anaweza kujiuliza sababu zake kama mipango ya kukabiliana na Ukimwi inapata mafanikio au watu wengine zaidi walioambukizwa wamefariki dunia. Mshiriki kutoka BAKWATA, Asina Shenduli akitoa maoni wakati wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.

 Naye Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mwitikio wa Kitaifa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Audrey Njelekela, alisema katika mkutano huo viongozi wa madhehebu mbalimbali nchini wanatarajiwa kutoka na mpango mkakati utakaohusisha mipango ya na taifa katika kampani ya kukabili Ukimwi. Alisema katika mkutano huo wa siku mbili, viongozi hao pamoja na kubadilishana uzoefu watapata nafasi ya kujifunza umuhimu wa kuratibu mapambano hayo ili kutumia vyema rasilimali watu na fedha zilizopo, Alisema pamoja na kuwepo kwa vikwazo katika shughuli za uratibu ikiwamo kukosekana kwa mtengamano na ukosefu rasilimali fedha, kuna faida kubwa ya kufanya uratibu kwa ajili ya kuwa na taarifa za uhakika na kutorudia kazi. Askofu Msaidizi wa AICT, Charles Sanagu (kushoto) akiuliza swali na kuwasilisha maoni katika mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.

 Alisema Tume ya kudhibiti Ukimwi ambayo ipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa kuita viongozi hao wa dini imelenga kufanya mapambano ya kukabili Ukimwi kuwa endelevu na yenye wigo mpana. Alisema katika mkutano huo pia walielezana kila kundi lipo wapi linafanya nini na kuimarisha uratibu dhidi ya ugonjwa huo. Naye Mwakilishi wa UNESCO katika mkutano huo, Herman Mathias ambaye pia ni Mratibu wa Ukimwi Unesco alisema kwamba mkutano huo pia una lengo la kutekeleza maazimio ya ESA ya mwaka 2013 ambapo nchi zinahamasishwa kutoa elimu kubwa kwa vijana wao kuhusu afya ya uzazi. Pichani juu na chini ni sehemu ya washiriki wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.
 Aidha mkutano utaangalia maelekezo kuhusu 2020 vijana kufikiwa na huduma rafiki za afya ya uzazi, kupunguza ndoa za utotoni, unyanyasaji kijinsia na ukeketaji. Alisema watu wa dini wana mchango mkubwa ndio maana Unesco kwa kushirikiana na Tume ya Ukimwi wameandaa mkutano huo ili kubadilisha mawazo na uzoefu. Ofisa mipango ya Elimu wa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tanzania, Jennifer Kotta (wa kwanza kushoto) akiwa na baadhi ya washiriki wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo. Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk. Leonard Maboko katika picha ya pamoja na washiriki wa mkutano wa kuimarisha uratibu wa Afua za Ukimwi katika Taasisi za Kidini uliofanyika Chuo cha Maendeleo na Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo kwa ufadhili wa UNESCO.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad