HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, December 16, 2017

TANROADS WATAKIWA KUSIMAMIA SHERIA

  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akikagua nguzo za daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 lililopo katika barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), yenye urefu wa KM 231.5, Mkoani Dodoma. Daraja hilo linaunganisha Wilaya ya Chemba na Kondoa mkoani humo.
Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Dodoma, Mhandisi Leonard Chimagu, akitoa maelezo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (katikati), kuhusu kazi zilizobaki katika barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), yenye urefu wa KM 231.5, wakati wa ukaguzi wa barabara hiyo iliyokamilika kwa asilimia 98.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (katikati), akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa ukaguzi wa barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), yenye urefu wa KM 231.5 iliyokamilika kujengwa kwa kiwango cha lami.
Muonekano wa sehemu ya wa barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), yenye urefu wa KM 231.5 iliyokamilika kujengwa kwa kiwango cha lami kwa asilimia 98. Kazi zilizobaki ni kuweka alama za barabarani.

Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), na Watendaji wa Mamlaka mbalimbali nchini wametakiwa kusimamia sheria ili kuhakikisha kuwa wanadhibiti changamoto za uharibifu wa miundombinu ya barabara.

Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa,  wakati akikagua barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), KM 231.5 ambapo amesema kuwa mamlaka zote hizo  zikishirikiana kwa pamoja katika suala zima la ulinzi na utekelezaji wa sheria kutasaidia miundombinu hiyo kudumu kwa muda mrefu.

"Vitendo kama vya umwagaji wa mafuta ya magari kwenye barabara, kupiga jeki, kuswaga wanyama, kuchimba kokoto na mchanga kwenye madaraja  vinachangia sana uharibifu  wa barabara, hivyo  simamieni kuhakikisha vitendo hivi vinakoma mara moja", amesisitiza Waziri Prof. Mbarawa.

Aidha, Profesa Mbarawa,amewataka madereva kufuata alama za kudhibiti mwendo (spidi) zilizoko barabarani hususani katika kipindi hiki cha sikukuu kwani kutokufuata sheria hiyo kunapelekea  ajali nyingi za barabarani. 
Katika hatua nyingine, Profesa Mbarawa ameipongeza TANROADS na Kampuni ya Mkandarasi ya CHICO kwa kuhakikisha kuwa barabara hiyo na daraja kubwa la Kelema lenye urefu wa mita 205 lililopo kwenye barabara hiyo linakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.

Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS mkoa wa Dodoma, Mhandisi Leonard Chimagu,  amesema kuwa barabara hiyo imekamilika kwa asilimia 98 ambapo  kazi zinazofanyika sasa ni uwekaji wa kingo na alama za barabarani hivyo  amefafanua kuwa kazi hiyo inatarajiwa kukamilika hivi karibuni.

Barabara ya Dodoma-Mayamaya-Mela-Bonga (Babati), yenye urefu wa kilometa 231.5 ambayo imejengwa kwa takribani shilingi Bilioni  257.6 inatarajiwa kufunguliwa mwakani na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad