HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 3, 2017

TSA yahitaji Sh milioni 66 kwa ajili ya mashindano ya Cana kanda ya tatu

Wakati mashindano ya kuogelea ya kanda  ya tatu ya Afrika (Cana zone 3) yamebakiza takribani wiki mbili kufanyika, Chama Cha kuogelea nchini (TSA) bado kinasaka kiasi cha fedha taslimu shilling milioni 66 ili kufanikisha mashindano hayo. Mpaka sasa, jumla ya nchi nane  zimethibitisha kushiriki katika mashindano hayo ambayo yanafanyika Tanzania kwa mara ya kwanza katika hisoria ya Tanzania. Mashindano hayo yamepangwa kuanza Oktoba 19 mpaka 21 kwenye bwawa la kuogelea la Hopac la jijini.

Katibu Mkuu wa TSA, Ramadhan Namkoveka alisema kuwa pamoja na maandalizi kuendelea vizuri chini ya mwenyekiti wa  Kamati ya mashindano,  Leena Kapadia, bado hawajatimiza lengo lao kukusanya fedha kwa ajili ya mashindano  hayo. Namkoveka alisema kuwa awali walikuwa wanahitaji Sh milioni 100, hata hivyo kiasi hicho cha fedha kimepungua kutokana na wadhamini mbalimbali kujitokeza kuchangia. Wadhamini hao ni pamoja na kampuni ya simu ya Vodacom Tanzania, Swissair, JCDecaux, , Label Promotions , Print Galore na Slipway Hotel.
“ Kamati  imeweza  kutafuta fedha kwa  makampuni 34 na bado tuna imani kati yao watajitokeza kusaidia gharama za maandalizi. Tunatoa wito kwa kampuni zilizopo ndani na nje ya nchi kudhamini mashindano haya ikiamini kuwa licha ya kujitangaza kwa biashara zao itasaidia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa mchezo wa kuogelea katika kanda ya Afrika ya Mashariki na Kati,” alisema Namkoveka.

Alifafanua kuwa viwango vya waogeleaji wa timu ya Taifa vinaendelea kuhimarika hasa kwa kutambua kuwa mashindano kwani  ni sehemu ya kujiandaa kwa mashindano ya Jumuiya Ya Madola yatakayofanyika Huko Australia Mwakani, Olimpiki ya Vijana ya Mwezi Oktoba, na Kufanyika Nchini Argentina.

Alisema kuwa mashindano haya ni sehemu ya maandalizi ya mashindano yatakatotumika kwa ajili kushiriki mashindano ya CANA kanda ya nne yatakayofanyika nchini Malawi. Wakati huo huo; Shirikisho la Mchezo wa Kuogelea la Dunia (FINA) watatoa dola za kimarekani 10,000 kusaidia gharama za maandalizi.

Namkoveka alitoa  shukrani kwa  Fina  kwa kusaidia kukua kwa mchezo huu hapa Duniani na hakika wanafanya kazi kubwa ya kusaidia mchezo huu kukua. Mchango wao huu utaleta ufanisi katika mashindano haya. Nchi zilizothibitisha kushiriki mashindano hayo ni nchi za Afrika ya Kusini, Zambia, Kenya, Uganda, Rwanda, Sudan ya Kusini, Djibout, na mwenyeji na  bingwa mtetezi nchi ya Tanzania.
Wakati huohuo, Chama Cha Kuogelea kimeamua kuimarisha usimamizi wa Timu ya Tanzania kwa kuteua Meneja wawili watakaoshughulikia timu ya Tanzania. Chama kimeamua kuteua mameneja wawili kwa kuwa nchi ya Tanzania kwa kuwa ni mwenyeji inaruhusiwa kuwa na timu mbili. Mameneja walioteuliwa ni Priscilla Zengeni na Jones Gouw. Waogeleaji wa Tanzania wapo chini ya makocha Alexander Mwaipasi na Michael Livingstone na baadhi ya wachezaji walioko mikoani wapo chini ya makocha wao wa Klabu au shule.

Alisema kuwa kuna changamoto ya kuweka kambi ya pamoja kwa kuwa wachezaji wanaounda timu hii wengine wanatoka Morogoro, Zanzibar, Arusha, Mwanza na Kilimanjaro na pia ni wachezaji ambao wako mashuleni wanakosoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad