HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 12, 2017

Rejesheni Uadilifu, Uzalendo Nchini- Ole Nasha

Jonas Kamaleki- MAELEZO
Serikali yawataka watanzania kurejesha nchi katika misingi iliyoachwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kuwa na viongozi waadilifu,wazalendo na wenye uchungu na nchi yao.
Wito huo umetolewa leo jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. William Ole Nasha wakati akifungua Kongamano la Kumbukizi ya Miaka 18 ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Ole Nasha amesema kuwa kumekuwa na ombwe kubwa la kuporomoka kwa maadili, kushamiri kwa rushwa, ufisadi, kukosekana kwa uzalendo na uwajibikaji, kuwepo kwa wafanyakazi hewa na biashara ya madawa ya kulevya.
Ameongeza kuwa wengi waliokuwa wakiharibu nchi hii ni watanzania wenyewe kwa ajili ya tamaa na ubinafsi wao.
“Nimefarijika sana kusikia kuwa Chuo kimeanza kurejesha hadhi yake iliyokuwepo hapo awali  kilipoasisiwa kwa kuanzisha program maalum ya Uongozi, Maadili na Utawala Bora,”alisema Ole Nasha.
Akizungumzia Mada Kuu ya Kongamano ambayo ni Mtazamo wa Mwalimu Nyerere katika Uchumi wa Viwanda na Maendeleo ya Jamii, Naibu Waziri amesema kuwa ni ukweli usiopingika katika uchumi wa maendeleo ya viwanda, Uzalendo, Utaifa, Uadilifu na Uongozi Bora vinapaswa kuzingatiwa.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku amesema kuwa viwanda si maendeleo bali ni matokeo ya maendeleo.
Amesema nchi inawezakuwa na viwanda lakini vinamilikiwa na wageni huku watanzania wakiwa manamba na vibarua. Hivyo amewataka wananchi wenyewe wajitahidi kuanzisha viwanda ambavyo vitatoa ajira kwa vijana wa kitanzania.
Butiku amesema kusema nchi imeendelea wakati bado kuna rushwa na kutokuwajibika huko sio kuendelea bado inahitaji kuendelea.
Akimzungumzia Mwalimu alisema kuwa Nyerere alisema huwezi kujenga viwanda bila kujali misingi. Misingi hiyo Butiku ameitaja kuwa ni kuhtambua kuwa Tanzania ni nchi ya watanzania, usawa wa binadamu msingi ambao Mwalimu alikuwa muumini.
Jambo ambalo limejitokeza kwa wingi katika Kongamano hilo ni msisitizo ulikuwa juu uzalendo, utaifa,uadilifu na uwajibikaji.
Kongamano hilo lilihudhuriwa na wanataaluma, wananchi wa kawaida, wanafunzi, wanavyuo na viongozi wastaafu akiwemo Spika wa Bunge Mstaafu, Anna Makinda, Ibrahim Kaduma, Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Prof. Mark Mwandosa na Viongozi wa Vyama vya Siasa akiwemo Prof. Ibrahim Lipumba na John Shibuda
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. William Ole Nasha

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad