HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, September 24, 2017

MKE WA TUNDU LISSU, DREVA WAKE WAFUNGUKA KWA MARA YA KWANZA

Kwa mara ya kwanza, Alicia Magabe ambaye ni mke wa Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amezungumzia tukio la mumewe kushambuliwa kwa risasi na kudokeza kwamba haliwezi kuwa limetokana na sababu nyingine isipokuwa kazi ambazo amekuwa akizifanya.

Pia amezungumzia kuhusu afya yake na kueleza kuwa bado siyo nzuri na kuwaomba Watanzania waendelee kumuombea.

Mbali ya Alicia ambaye pia ni mwanasheria, dereva wa Lissu naye amezungumza akisema ameathiriwa kwa kiasi kikubwa na tukio hilo huku akiahidi kuripoti polisi mara baada ya kurejea nchini.

Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), amelazwa katika Hospitali ya Nairobi tangu alipopelekwa huko baada ya kupigwa risasi akiwa ndani ya gari nje ya nyumba yake mjini Dodoma mchana wa Septemba 7 akitokea bungeni.

“Watanzania wote wanajua Lissu maisha yake yote amekuwa ni mtetezi wa wanyonge na tukio hili amelipata kutokana na kazi zake hizo hivyo nawaomba tumuombee tu,” alisema.

“Ninachoweza kusema hali ya mheshimiwa Lissu sio nzuri ingawa ni tofauti na tulivyomleta hapa, hivyo naomba Watanzania kuendelea kumuombea.”

Aliwashukuru Watanzania kwa michango, na maombi yao kwa Lissu akisema hiyo inaonyesha ni jinsi gani wanathamini mchango wake kwa jamii.

Alipoulizwa kuhusu kauli ya Serikali kwamba ipo tayari kugharimia matibabu ya Lissu popote ikiwa itaombwa na familia hiyo, Alicia ambaye pia ni wakili alisema kwa sasa hana maoni.

“Katika hili no comment (sina maoni) ndio tumesikia jana amezungumza na kwa kuwa jambo hili siyo la uamuzi wa mtu mmoja, mimi sina cha kusema,” alisema.

Hata hivyo, alisema anashukuru kazi kubwa ambayo inafanywa na madaktari wa Hospitali ya Nairobi na kusema wanaridhishwa na matibabu ambayo anapatiwa kwa sasa.

Kauli  ya  Dereva wa Lissu
Mbali ya Alicia, dereva wa Lissu ambaye ndiye mtu pekee waliyekuwa wote siku ya tukio hilo, Simon Bakari naye alizungumza kwa mara ya kwanza kuhusu tukio hilo na kudokeza kwamba limevuruga na hana kumbukumbu sahihi.

Dereva huyo ambaye naye anaendelea kupatiwa matibabu ya kisaikolojia katika hospitali hiyo ya Nairobi alisisitiza, “Kwa sasa siwezi kuzungumza vizuri tukio hili kwani nadhani sina kumbukumbu vizuri.”

Alipoulizwa kuhusu wito wa polisi wa kwenda kutoa maelezo, alisema atafanya hivyo pindi atakaporejea nchini baada ya matibabu.

“Nilisikia polisi wamenitaka nikatoe maelezo lakini sijisikii vizuri na bado napata matibabu. Nitakwenda,” alisema.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad