HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, August 27, 2017

WAZIRI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA MAKAMU WA RAIS WA CUBA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano. katika Mji wa Havana Nchini Cuba jana August 26/2017. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akifanya mazungumzo ya Kikazi na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano. katika Mji wa Havana Nchini Cuba jana August 26/2017. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu


*Asisitiza nia ya kufungua ubalozi nchini humo
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano na kumuhakikishia ufunguzi wa ofisi za ubalozi wa Tanzania nchini humo.

Amesema Tanzania inayatambua na kuyathamini mahusiano mazuri ya kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi, kielimu, kiafya na kiutamaduni kati yake na Cuba, hivyo inatarajia kufungua ubalozi nchini humo ili kurahisisha utendaji wa kazi za kibalozi.

Waziri Mkuu alikutana na Bi. Gladys jana jioni (Jumamosi, Agosti 26, 2017) wakati alipokuwa akihitimisha ziara yake ya kikazi nchini Cuba. Malengo ya ziara yalikuwa ni kuimarisha na kudumisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

“Tunatambua mahusiano mazuri yaliyopo kati Tanzania na Cuba, ambayo yalikuwepo kuanzia Serikali ya Awamu ya kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Nyerere, hivyo lazima tufungue ofisi za ubalozi na tutamleta balozi wetu hapa.”

Pia Waziri Mkuu ameishukuru Serikali ya Cuba kwa ujenzi wa kiwanda cha dawa za kuulia vijidudu vya maralia pamoja na ufadhili wa masomo ya udaktari inaoutoa kwa wanafunzi wa Kitanzania ambao wanasoma katika vyuo mbalimbali nchini humo.

Hata hivyo aliiomba Serikali hiyo iendelee kutoa ufadhili wa masomo kwa madaktari hao hadi ngazi ya shahada ya uzamili kwa sababu Serikali ya Tanzania inawahitaji madaktari bingwa wengi kwani walioko nchini ni wachache.

Kwa upande wake, Bi. Gladys alimshukuru Waziri Mkuu kwa kufanya ziara nchini Cuba na alimuhakikishia kwamba uhusiano wa Serikali yake na Serikali ya Tanzania utaendelea kuimarishwa kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.

Alisema Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Magufuli inafanya jitihada kubwa za kuhakikisha uchumi wake unakua kwa kasi jambo ambalo ni tofauti na mataifa mengine. “Nawapongeza kwa hatua za kimaendeleo mnazozifanya.”

Makamu huyo wa Rais alisema Serikali ya Cuba itaendelea kushirikiana na Tanzania katika uboreshaji wa Sekta za Afya, Utamaduni, Kilimo, Uchumi na Elimu. Kuhusu ombi la kuongeza ufadhili wa shahada ya uzamili kwa madaktari  alisema amelipokea na atalifanyia kazi.

Awali Balozi wa Tanzania nchini Canada, ambaye anasimamia na nchi ya Cuba, Balozi Jack Zoka alisema Serikali ya Cuba ni miongoni mwa nchi zinazoshirikiana na Tanzania katika uboreshaji wa shughuli za maedndeleo, hivyo uwepo wa ofisi za ubalozi nchini humo utazidi kuimarisha mahusiano.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad