HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 11, 2017

Waziri Lukuvi kugawa hati za ardhi 2,111 Kilombero, Morogoro

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Programu ya Kuwezesha Umilikishaji Ardhi (Land Tenure Support Programme - LTSP) itazindua rasmi utoaji wa Hati za Hakimiliki ya Kimila katika kijiji cha Nyange, wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro tarehe 15 Agosti, 2017.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi atakuwa mgeni rasmi katika tukio hilo ambapo atagawa hati 2,111 kwa wananchi wa kijiji cha Nyange na kuzindua ofisi na masjala ya ardhi ya kijiji hicho. Ofisi na masjala ya ardhi ya kijiji cha Nyange imejengwa kwa nguvu za wananchi na msaada wa Serikali kupitia mradi wa LTSP.


LTSP ni Programu iliyo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Programu hii ni mahsusi kwa wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi ambapo takribani vijiji 160 vitanufaika. Hadi sasa, Programu imehakiki na kupima vipande vya ardhi 21,154 katika vijiji 18 vya Wilaya za Kilombero na Ulanga. Kati ya vipande vilivyohakikiwa na kupimwa, jumla ya vipande 9,112 vimeandaliwa Hati za Hakimiliki ya Kimila.


Kazi nyingine zilizotekelezwa na Programu ni pamoja na:


Kusimika alama za msingi 54 za mtandao wa kijiodesia katika Wilaya za Kilombero, Ulanga, Malinyi na Mufindi;

Kupima mipaka ya vijiji 50 na kutatua migogoro 18 ya mipaka ya vijiji iliyodumu kwa muda mrefu;
Kuandaa vyeti vya Ardhi ya Kijiji kwa vijiji 57;
Kuandaa mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Vijiji kwa vijiji 50; na
Kuchangia katika ujenzi na ukarabati wa masjala za ardhi na ofisi za vijiji katika vijiji 61.
Wadau mbalimbali, wakiwemo washirika wa maendeleo wanaofadhili Programu ya LTSP na wananchi watashiriki katika uzinduzi huo.

Programu hii inafadhiliwa na mashirika ya maendeleo ya DFID, DANIDA na SIDA. Wananchi wote wanakaribishwa kushuhudia tukio hili.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad