HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, August 28, 2017

Polisi Singida waua mtu mmoja akidaiwa kuwa jambazi

Mkazi wa kijiji cha Shiponga, Hanang Mkoani Manyara anayedaiwa kuwa jambazi, Hamisi Athumani (32), amefariki dunia baada ya kupigwa risasi kiunoni na askari polisi wakati akiwa katika harakati ya kutoroka.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani hapa, ACP Debora Magiligimba, amesema tukio hilo limetokea Agosti 25 mwaka huu saa nane mchana, huko katika kijiji cha Mgori tarafa ya Ngimu wilaya ya Singida.
Amefafanua kuwa Hamisi (marehemu) alipigwa risasi na askari polisi wakati akijaribu kuwatoroka mara baada kuonyesha bunduki aina ya rifle yenye namba 7358 na risasi zake tano.

Amesema bunduki hiyo iliyokuwa imekatwa mtutu na risasi zake tano zilikuwa zimefichwa kwenye soksi, vitu hivyo vilikuwa vilihifadhiwa kwenye mfuko wa sandarusi, na kufichwa chini ya jiwe.

ACP Magiligimba amesema Agosti 23 mwaka huu, mtuhumiwa alikamatwa na wananchi wa kijiji cha Ngamu, na kufikishwa katika kituo cha polisi cha kijiji hicho kwa tuhuma ya kujihusisha na matukio ya ujambazi.

“Kesho yake mtuhumiwa alihojiwa na kukiri kujihusisha na matukio ya ujambazi wa kutumia silaha katika mikoa mbalimbali. Pia aliahidi kuwapeleka askari kuwaonyesha mahali alikoificha silaha anayoitumia kwenye matukio hayo ya ujambazi,” amesema ACP Magiligimba.

Kamanda huyo amesema Agosti 25 mwaka huu saa sita mchana, askari polisi wakiwa na mtuhumiwa, walikwenda katika pori la kijiji cha Mgori mahali alipokuwa ameficha bunduki hiyo aina ya rifle.

“Mara tu baada ya kuwaonyesha askari hao silaha hiyo na wakati askari wanaendelea kufanya upekuzi katika eneo hilo, mtuhumiwa alijaribu kutoroka askari kwa kukimbia” amesema na kuongeza.

“Askari mmoja alifyatua risasi tatu hewani akimtaka asimame, lakini hakutii. Ndipo alipompiga risasi moja iliyompata sehemu ya kiunoni”.

Amesema jereha hilo la risasi lilisababisha mtuhumiwa Hamisi avuje damu nyingi, na hivyo kufariki dunia wakati akikimbizwa hospitali ya mkoa kwa matibabu.

“Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida linaendelea kutoa wito kwa wananchi waote kutoa taarifa zitakazosaidia kubaini wahalifu katika maeneo yao ili hatua ziweze kuchukuliwa kudhibiti vitendo vya kihalifu,” amesema kamanda huyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad