HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 22, 2017

Mwili wa mwanaharakati wa tembo aliyeuawa kwa risasi kuagwa leo jijini Dar

Mwili wa mwanaharakati wa kupinga ujangili na biashara haramu ya meno ya tembo wa nchi za Afrika Wayne Lotter, aliyepigwa risasi na kuuawa jijini Dar es Salaam Jumatano iliyopita unatarajiwa kuagwa leo katika viwanja vya Baobao Villlge Masaki jijini Dar.
Wayne ambaye alikuwa mwanzilishi wa PAMS Foundation, taasisi ambayo imekuwa katika mstari wa mbele kusaidia kupambana na uwindaji haramu na biashara ya pembe za ndovu nchini Tanzania aliuawa na watu wasiofahamika Agosti 16 mwaka huu wakati anatoka Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere akielekea nyumbani kwake Masaki.
Akizungumza na wana habari kwa niaba ya wana familia, jana Krissie Clark alisema wanatarajia kuuaga mwili wa mwanaharakati huyo leo kisha kuusafirisha kwenda nyumbani kwao Afrika Kusini kwa maziko.
Alisema kuuawa kwa Wayne hakutawafanya kurudisha nyuma mapambano dhidi ya ujangili na badala yake wameelekeza nguvu zao katika Afrika ili kutokomeza kabisa ujangili kama ilivyokuwa ndoto ya ndugu yao.
Kifo cha mwanaharakati huyo kimeacha maswali mengi yasiyokuwa na majibu hasa ikizingatiwa kuwa amesaidia kwa kiasi kikubwa kukamatwa kwa vinara wengi wa ujangili akiwemo Malkia wa Meno ya Tembo.
Kifo chake kimetikisa mataifa ya nje ya bara hili la Afrika kwani magazeti ya New York Times la Marekani na The Guardian na The Independent ya Uingereza yamekuwa yakimtaja kwamba enzi za uhai wake alitetea wanyama hasa tembo ambao wamekuwa wakiwindwa na majangili, hivyo kuwa mmoja wa waliosaidia kukamatwa kwa watuhumiwa wa ujangili nchi mbalimbali Tanzania ikiwemo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad