HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 11, 2017

FAHAMU VISIMA VYA UZIMAJI MOTO (fire hydrants)

WATU wengi wamekuwa wakikuta na kuvipita vifaa mithili ya mabomba ya kutoa maji pembezoni mwa barabara, maeneo yenye mkusanyiko mkubwa wa watu, viwanja vya ndege au viwanja vya michezo bila kufahamu vinafanya kazi gani.

Wengine hudhani ni mapambo ya barabara au alama Fulani kwenye maeneo hayo, ambapo baadhi yao hudiriki kuyatumia kinyume na kazi yake kutokana na kutotambua matumizi yake.

Mabomba haya (fire hydrants) sio mapambo bali ni mfumo uliounganishwa na mabomba makubwa ya maji, na kuwa visima vya maji ambapo gari la Zimamoto huchukua maji. Visima hivi vimejengwa makusudi kwa ajili ya kulirahisishia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kukabiliana na majanga ya moto pindi yanapotokea.

Mabomba hayo (Fire Hydrant) yana msukumo mkubwa wa maji na kusababisha maji yatoke kwa wingi na kwamuda mfupi. Uwepo wa vifaa hivyo sehemu mbalimbali za makazi ya watu na maeneo mengineyo hurahisisha zoezi zima la uzimaji moto, kwani pindi gari la kuzima moto linapoishiwa maji hujazwa hapohapo badala ya kuyafuata mbali na eneo la tukio.

Kwa kawaida magari ya zimamoto yana ujazo tofauti wa maji kuanzia lita 2000 hadi lita 16,000 ambapo ni ujazo mkubwa zaidi. Magari haya hubeba maji ya awali kwa ajili ya huduma ya kwanza ndio maana visima hivyo ni muhimu kuwepo.

Kwa nini tunasema ni maji kwa ajili ya huduma ya kwanza, ni kwa sababu ujazo wa maji yanayobebwa na gari la zimamoto ambao ni kati ya lita 2000 na lita 16000, hutoka kwamsukumo mkubwa, ambao kwa dakika moja maji yatatoka zaidi ya lita 1000 ukiwa unatumia mstari mmoja wa mpira wa maji (hose) na kusababisha maji hayo kuisha kwa muda mfupi.

Ukosefu wa visima hivyo sehemu mbalimbali, unapelekea Jeshi kushindwa kukabiliana na majanga ya moto kwa ufanisi baada ya maji yanayokuwa kwenye gari kuisha na kuwalazimu kwenda eneo la mbali.

Ingawa Jeshi la zimamoto na uokoaji linajitahidi kadri iwezekanavyo kuhakikisha linakabiliana vya kutosha na majanga ya moto kwa kusambaza visima hivi vya maji, lakini marakadhaa limekuwa linakumbana na changamoto mbalimbali hasa miundombinu.

Katika kuhakikisha tatizo hilo linatatuliwa, tayari baadhi ya Mikoa kama vile Dar es Salaam, Mbeya, Kilimanjaro, Arusha na Tanga imejitahidi kuhakikisha miundombinu yake inakidhi kuruhusu ujenzi wa visima vya maji ya kuzimia moto na utaratibu umeandaliwa kuhakikisha mikoa Mingine inaboresha miundombinu yake kwa kuzingatia ujenzi wa huduma hiyo.

Pamoja na changamoto hizo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji bado linatekeleza wajibu wake kwa kuwa elimisha wananchi namna ya kutunza miundombinu hiyo na kusambaza mifumo hiyo kwa kiwango kinacho hitajika.

Wito kwa wananchi tuyatunze mabomba hayo (fire hydrant) kutokana na kuwa na umuhimu katika kurahisisha shughuli za kupambana na majanga ya moto, kwani kumekuwa na wimbi kubwa la uuzaji wa vyuma chakavu.
Web site: www.frf.go.tz

IMEANDALIWA NA KITENGO CHA HABARI NA ELIMU KWA UMMA-MAKAO MAKUU YA JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad