KATIKA kuhakikisha inarahisisha upatikanaji wa huduma ya majisafi na kwenda na
mfumo wa kisasa wa mawasiliano ya kiteknolojia, Shirika la MajiSafi na Majitaka Dar es
Salaam (DAWASCO) limezindua mfumo mpya wa mawasiliano ambao unalenga
kumrahisishia mteja kupata na kutoa taarifa zinazohusu huduma hiyo kwa haraka zaidi.
Huduma hiyo mpya sasa itapatikana kwa wakazi wote wa jiji la Dar es Salaam na Mkoa
wa Pwani. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa
Mawasiliano na Teknolojia (TEHAMA) wa
DAWASCO, Kiula Kingu amesema lengo kuu la mfumo huu ni kumweka mteja
karibu kihuduma na kila mwananchi ana uwezo wa kutumia mfumo huo katika simu
yake kupitia mitandao yote ya simu za mikononi nchini.
Mkurugenzi
wa
Mawasiliano na Teknolojia (TEHAMA) wa
DAWASCO, Kiula Kingu akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es
salaam wakati akitangaza uwepo wa mfumo mpya wa mawasiliano ambao
unalenga
kumrahisishia mteja kupata na kutoa taarifa zinazohusu huduma hiyo kwa
haraka zaidi. Kushoto ni Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Everlasting Lyaro.
Kingu ameongeza kuwa ili mteja kunufaika na mfumo huu anatakiwa kuhakikisha ana
simu ya mkononi ya “Smartphone” ambayo itamwezesha kupakua mfumo huo mpya wa
DAWASCO, kisha kujisajili kwa kuingiza akaunti namba yake ya DAWASCO ambapo
baada ya kufuata hatua zote za kujisajili mteja atatumiwa neno la siri ambalo
litamwezesha kuingia na kupata taarifa husika. “Sisi Dawasco tumeona haja ya
kujiboresha na kwenda sawa na teknolojia kwa kumletea mteja wetu mfumo rahisi
ambao utamwezesha kupata taarifa zetu kupitia simu yake ya mkononi muda
wowote,”alisema Kingu.
Naye, Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Everlasting Lyaro, amewataka wananchi wa
Dar es Salaam na Pwani kupakua mfumo huu kwani ni rahisi kuutumia na hauna
gharama zozote. Anasema ni mfumo ambao utamrahisishia mteja kupata taarifa
muhimu zinazohusu huduma ya maji zikiwamo ankara ya mwezi, taarifa za lini mteja
alifungiwa huduma ya maji, muda ambao alifanya malipo, lini mita yake ya maji
ilisomwa na taarifa nyingine nyingi.
“Nawasihi wateja wetu na wananchi wote kupakua mfumo huu mpya katika simu zenu
za mkononi ili kuweza kufurahia huduma zetu, hakuna gharama zozote ambazo
utatozwa. Kupitia mfumo huu utaweza kupata taarifa zote muhimu za huduma ya
majisafi zikiwemo taarifa za mivujo ya maji na ankara za maji za kila
mwezi,”amefafanua Lyaro.
Anasema kwa sasa wateja hawana haja ya kutumia muda mrefu katika ufuatiliaji wa
kuunganishwa huduma ya maji, bali kilichorahisishwa ni mteja kuweka taarifa zake
sahihi kwenye mfumo huo na DAWASCO itatumia taarifa hizo kumtafuta mteja na
kukamilisha taratibu nyingine hadi kuhakikisha mteja anapata huduma ya maji.
Katika kutimiza agizo la Waziri wa Maji na Imwagiliaji, Mhandisi Greyson Lwengwe la
kuhakikisha wakazi wa Dar es salaama, Miji ya Kibaha na Bagamoyo wanapata huduma
ya maji safi, DAWASCO imekua ikijitahidi kuwafikia wananchi kwa njia na mbinu tofauti,
kampeni tofauti kama 'mama tua ndoo ya maji kichwani' huku maunganisho ya maji
kwa mkopo yakisaidia upatikanaji na uboreshaji wa huduma ya maji kwa maeneo mengi
ya jiji la Dar es Salaam.
Mpaka sasa takribani watumiaji 25,000 wa mitandao ya simu jijini Dar es Salaam
wameshapakua mfumo huu na lengo la DAWASCO ni kuwafikia wakazi wengi zaidi kwa
kipindi kifupi.
No comments:
Post a Comment