HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, July 26, 2017

WAZIRI WA AFYA AMSIMAMISHA KAZI MGANGA MFAWIDHI WA KITUO CHA AFYA MLANDIZI KWA KUSHINDWA KUSIMAMIA MAAGIZO YA SERIKALI


Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha

WAZIRI wa afya, jinsia, wazee na watoto, Ummy Mwalimu amemsimamisha kazi mganga mfawidhi wa kituo cha afya Mlandizi, Dk. Mpola Tamambele, kutokana na kushindwa kusimamia maelekezo ya serikali ya kuhakikisha mama mjamzito, mtoto chini ya miaka mitano na mzee wanapata huduma bure.

Kutokana na kutokuwa na mamlaka ya moja kwa moja amemuagiza Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya halmashauri ya wilaya ya Kibaha, Beda Mmbaga kumsimamisha kazi mganga mfawidhi huyo mara moja wakati uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili zikiendelea .

Amemuelekeza Kaimu Mkurugenzi huyo pia kuwafuatilia watumishi wa afya kituoni hapo waliohusika kumuagiza mama aliyejifungua Salma Khalifan kwenda kununua vifaa vya kujifungulia vya sh.180,000 ili apate huduma .

Aliyasema hayo wakati alipokwenda kutembelea kituo cha afya Mlandizi, kabla ya kukabidhiwa kwa magari ya wagonjwa matatu kutoka kwa mbunge wa jimbo hilo, Hamoud Jumaa.

Waziri huyo alisema yeye hana mamlaka ya moja kwa moja kumsimamisha kazi mganga mfawidhi huyo hivyo anaiachia mamlaka husika isimamie jukumu hilo. Alisema hatokubali kuona watumishi wachache kwenye vituo vya afya, zahanati na hospitali wanachezea maagizo ya serikali. Alifikia hatua hiyo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa mama aliyejifungua ambae alisema amenunua vifaa vya kufanyiwa operesheni kwa gharama ya sh .180, 000.
Ummy alisema haiwezekani kuona mama wajawazito, wanalipishwa hadi gloves na pamba ili kujifungua wakati serikali yao ilishasema watahudumiwa bure . Alieleza kwamba, kuanzia sasa waganga wakuu wa wilaya, mikoa na watumishi wa afya wote nchini wahakikishe wanatimiza maelekezo ya serikali kuhudumia akinamama wajawazito na watoto ili kupunguza vifo vya uzazi . Ummy alisema kuwa ,watumishi na wauguzi wengi wanajituma na kufanya kazi zao kifanisi ila wapo wachache ambao wanakwamisha juhudi hizo .

"Sitokubali mtumishi anakwenda kinyume na serikali ,rais wetu John Magufuli anasisimamia suala zima la kuboresha huduma za afya ,halafu akitokea mtu mmoja mzembe anatuchanganya kwakweli sitoweza kumfumbia macho "

"Wananchi wamekuwa waoga hata kuingia katika suala la bima ya afya kwa sababu ya mambo kama haya ,namsimamisha mganga mfawidhi huyo hadi hapo uchunguzi utakapokamilika ." alisema Ummy .

Mbali ya hayo Ummy alibainisha,bajeti ya dawa katika halmashauri ya  wilaya ya Kibaha imeongezeka ndani ya miaka miwili mfululizo kwenye uongozi wa serikali ya awamu ya tano .
Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akitembelea kituo cha afya Mlandizi katika ziara yake aliyoifanya jana. kushoto ni Mganga Mfawidhi wa kituo cha afya Mlandizi, Dk. Mpola Tamambele, ambaye amesimamishwa kazi kupisha uchunguzi.

Ummy alisema mwaka 2015/2016 bajeti ya madawa katika halmashauri hiyo ilikuwa mil.24 na 2017 ilifikia mil.70 na bajeti ya sasa 2017/2018 imefikia sh. mil.101 .

Kwa upande wake mama aliyejifungua kituoni hapo ,Salma Khalfani ,alimweleza Ummy kwamba aliandikiwa orodha ya dawa za kununua kwenye maduka ya dawa ya nje .

Alieleza ,alitakiwa kufanyiwa upasuaji na hivyo kutakiwa kununua madawa na vifaaa tiba ,pamba na gloves vya 180,000 akanunue ili aweze kujifungua .

Kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo ,Mmbaga alisema maagizo aliyopewa na waziri ameyapokea na atayafanyia kazi .

Nae mbunge wa jimbo la Kibaha Vijijini, Hamoud Jumaaa alisema kumekuwa na malalamiko mengi juu ya wananchi hasa akinamama kulipishwa fedha za dawa na vifaa tiba. Alisema baadhi ya wazee wamekuwa wakishindwa kupewa huduma za afya bila malipo. Jumaa alimuomba Ummy kuendelea kushirikiana nae kuwadhibiti watumishi wazembe wanaodidimiza haki za wananchi .

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad