HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, July 17, 2017

PROF. MBARAWA AWATAKA TBA KUMALIZA NYUMBA YA JAJI MFAWIDHI

 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto), akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Bi. Zainab Tellack, mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ziara ya kikazi.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto), akifafanua jambo kwa viongozi wa Taasisi zilizopo chini ya Wizara alipokutana nao mkoani humo kwa ziara ya kikazi.
 Meneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), mkoa wa Shinyanga Eng. Amosi Manyete akimuonesha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, mfumo wa maji taka uliowekwa nje ya jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, kanda ya Shinyanga iliyopo mkoani humo. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda hiyo Mhe. Jaji Richard Kibella.
 Muonekano wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga ambalo limekamilika na ujenzi wake umesimamiwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akikagua moja ya nyumba za watumishi eneo la Rubaga zinazojengwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), mkoani Shinyanga.
Muonekano wa jengo la Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ambalo ujenzi wake unasimamiwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ameutaka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), kuhakikisha ndani ya miezi sita wanakamilisha ujenzi wa nyumba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga.
Prof. Mbarawa ametoa agizo hilo mkoani humo wakati alipokagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wakala huo ambapo pamoja na mambo mengine amesisitiza umuhimu wa kuwapatia waheshimiwa majaji mahali pazuri pa kuishi ili waweze kutimiza wajibu wao wa kutenda haki kwa wananchi ipasavyo.
“Hakikisheni mnakamilisha ujenzi wa nyumba hii haraka iwezekanavyo ili Mheshimiwa huyu apate mahali pazuri pa kuishi, kufanya hivi kutarahisisha majukumu yake na kufanikish utendaji wa kazi”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Amesisitiza umuhimu wa Wakala huo kuongeza kasi katika miradi mbalimbali inayoendelea ya ujenzi wa nyumba za viongozi ili kuondoa adha ya kodi za pango kubwa zinazopotea kwa viongozi hao kupanga kwa watu binafsi.
Naye, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Shinyanga Mhe. Jaji Richard Kibella amemshukuru Prof. Mbarawa kwa niaba ya taasisi zake za TBA na Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), kwa namna ambavyo wameshirikiana na Mahakama kukamilisha ujenzi wa jengo hilo na kuwapatia huduma nyingine za uendeshaji.
Aidha, ameiomba Serikali kukamilisha kwa haraka ujenzi wa nyumba za viongozi na watumishi wa mahakama kwani gharama kubwa zinatumika katika malipo ya upangaji wa nyumba za viongozi.
“Mhe. Prof. Mbarawa suala la nyumba ni changamoto, nyumba za kupanga zina gharama kubwa ambapo kwa namna moja au nyingine inaongeza gharama za uendeshaji wa mahakama na kupunguza usalama”, amefafanua Jaji Kibella.
Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama hiyo Bwana Ernest Masanja, amemueleza Prof. Mbarawa kuwa kukamilka kwa jengo la Mahakama hiyo kumewezesha Majaji na watendaji wengine wa mahakama kufanya kazi kwa bidii, ufanisi na kwa wakati katika kuwapatia wananchi haki. 
Katika hatua nyingine, Prof. Mbarawa ametembelea na kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Mkoa huo unaosimamiwa na TBA na ameuelekeza Wakala huo kushirikiana na Mamlaka husika kuhakikisha kuwa ujenzi wake unazingatia viwango na ubora na kukamilika kwa wakati.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad