HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, June 30, 2017

WAHALIFU WANNE WAUWAWA KATIKA MAPAMBANO NA POLISI KIBITI

Na Frank Geofray-Jeshi la Polisi.

Jeshi la Polisi nchini limefanikiwa kuwaua wahalifu wanne wanaosadikiwa kuwa miongoni mwa wahalifu wanaoendesha mauaji katika wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji  katika mapambano yaliyodumu kwa zaidi ya nusu saa katika kijiji cha Pagae wilayani Kibiti mkoani Pwani.

Akielezea tukio hilo Mkuu wa Oparesheni Maalumu za Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi Liberatus Sabas alisema tukio hilo lilitokea siku ya Alhamisi juni 29 majira ya saa tatu usiku kwenye barabara ya vumbi itokayo Pagae kuelekea Nyambunda ambapo Askari Polisi wakiwa doria walikutana na kikundi cha watu kinachokadiriwa kuwa na watu sita ambapo wahalifu hao baada ya kuona gari la Polisi walikimbilia vichakani na kuanza kuwarushia risasi Polisi.

Sabas alisema baada ya hali hiyo kutokea Askari nao kwa ujasiri walijibu  na mapambano hayo yalidumu kwa zaidi ya nusu saa ambapo Polisi walifanikiwa kuwajeruhi wahalifu wanne kwa risasi ambao baadaye walifariki dunia wakiwa wanapelekwa hospitali.

“Katika tukio hilo tumefanikiwa kupata silaha mbili aina ya SMG na magazine mbili pamoja na risasi 17 zilizokuwa zinatumiwa na wahalifu hao na hii ni dalili kuwa tunaendelea vizuri na oparesheni yetu ambayo inashirikisha vyombo vingine vya ulinzi na Usalama katika wilaya hizi tatu za Mkuranga, Kibiti, na Rufiji” Alisema Sabas.

Aidha Sabas ametoa wito kwa wahalifu wengine kuacha mara moja kufanya vitendo hivyo kwa kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kufanya jitihada zote za kuhakikisha kuwa maeneo hayo yanakuwa salama na wananchi wanaishi katika hali ya amani na usalama.

Vilevile amewataka wananchi kutoa taarifa zitakazowezesha kupatikana wahalifu wengine ili kuhakikisha kuwa kila mmoja anaishi kwa usalama ambapo kwa ambaye atakayetoa taarifa zitakazowezesha kupatikana kwa wahalifu hao kiasi cha shilingi milioni kumi kitatolewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro.
Mkuu wa Operesheni za Polisi, Naibu Kamishna DCP Liberatus Sabas, akionyesha bunduki aina ya smg zilizopatikana juzi usiku wakati wa mapambano ya kurushiana risasi baina ya wahalifu na polisi katika kijiji cha Pagae wilayani Kibiti mkoani Pwani. Bunduki 2 aina ya smg zilipatikana pamoja na magazini 2 na risasi 17. Picha na hassan mndeme-jeshi la polisi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad