Na Veronica Kazimoto, Morogoro
Uratibu wa Mfumo wa Taifa wa Takwimu umesaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha
uzalishaji takwimu rasmi nchini.
Hayo yamebainishwa na Mratibu wa Mpango Kabambe wa Kuboresha na Kuimarisha
Takwimu nchini, Philemon Mahimbo wakati wa mafunzo kwa Wanasheria wa Wizara na
Taasisi za Serikali kuhusu Sheria mpya ya Takwimu No. 9 ya Mwaka 2015 yaliyofanyika
leo mkoani Morogoro.
Mahimbo amesema mfumo huu unaoratibiwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa mujibu
wa Sheria ya Takwimu Na 9 ya mwaka 2015, umeweza kusaidia upatikanaji wa takwimu
rasmi ambazo zinatumika katika kupanga na kutekeleza miradi mbalimbali ya
kimaendeleo na kupunguza changamoto ya kukinzana kwa takwimu zilizokuwa
zinatolewa na taasisi mbalimbali.
Kwa upande wake Mwanasheria wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Oscar Mangula
amesema Sheria mpya ya Takwimu No. 9 ya Mwaka 2015 haimzuii mtu ama taasisi
kufanya utafiti bali inamtaka mtu au taasisi kuwasiliana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu
kupata kibali na miongozo kama anataka takwimu anazozikusanya ziwe rasmi.
“Sheria hii mpya ya Takwimu No. 9 ya Mwaka 2015 sio kwamba inazuia watu ama
taasisi kuendesha shughuli za utafiti au za kukusanya takwimu kwa matumizi ya mtu
binafsi au taasisi husika nchini bali inawataka kutumia miongozo kutoka Ofisi ya Taifa
ya Takwimu ili takwimu wanazozikusanya ziwe rasmi,” amesema Mangula.
Oscar Mangula amebainisha kuwa ni kosa kisheria kwa mtu ama taasisi kuendesha
utafiti wenye miongozo isiyothibitishwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu na kuzitangaza
kama takwimu rasmi.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu imepewa mamlaka kisheria ya kuratibu, kusimamia,
kuchambua na kusambaza takwimu rasmi nchini.
Mratibu wa Mpango Kabambe wa Kuboresha na
Kuimarisha Takwimu nchini (Tanzania Statistical Master Plan-TSMP) kutoka
Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Philemon Mahimbo akiwasilisha mada wakati wa
mafunzo kwa wanasheria kuhusu sheria mpya ya Takwimu ya Mwaka 2015
yaliyofanyika leo mkoani Morogoro.
Meneja wa Idara ya Mbinu za kitakwimu, Viwango na
Uratibu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Emilian Karugendo akiwasilisha
mada kuhusu takwimu na takwimu rasmi wakati wa mafunzo kwa
wanasheria kuhusu sheria mpya ya Takwimu ya Mwaka 2015 yaliyofanyika
leo mkoani Morogoro.
Baadhi ya wanasheria kutoka Wizara na taasisi za
Serikali wakifuatilia kwa makini uwasilishwaji wa mada zinazohusu sheria
mpya ya Takwimu ya Mwaka 2015 wakati wa mafunzo kwa wanasheria
kuhusu sheria hiyo yaliyofanyika leo mkoani Morogoro.
Baadhi ya wanasheria kutoka Wizara na taasisi za
Serikali wakifuatilia kwa makini uwasilishwaji wa mada zinazohusu sheria
mpya ya Takwimu ya Mwaka 2015 wakati wa mafunzo kwa wanasheria
kuhusu sheria hiyo yaliyofanyika leo mkoani Morogoro.
No comments:
Post a Comment