Hospitali Teule ya Mkoa wa Geita ambapo mpango unaoendeshwa na Mfuko wa Taifa wa Bima
ya Afya za huduma za Madaktari Bingwa.
Na Grace Michael, Geita
Mamia ya wananchi mkoani Geita wamejitokeza kupata huduma za madaktari
bingwa , mpango unaotekelezwa kwa ushiriiano wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya
Afya na Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Mpango huo ulianza kutekelezwa siku ya Jumatatu wiki hii, katika mikoa ya Geita
na Kigoma na unalenga kuwahudumia wagonjwa ambao wanahitaji huduma za
kibingwa ambazo hazipo katika Hospitali hizo.
Madaktari bingwa wanaoshiriki katika mpango huo ni wa magonjwa ya watoto,
mfumo wa mkojo, magonjwa ya ndani na moyo, magonjwa ya pua, masikio na
koo pamoja na huduma za dawa za usingizi na huduma za wagonjwa mahututi.
Wakizungumza katika uzinduzi wa mpango huo uliofanyika katika viwanja vya
hospitali ya mkoa wa Geita, wananchi waliojitokeza kupata huduma hizo
wamesema ujio wa wataalamu hao umekuwa msaada mkubwa na
umewaondolea usumbufu na gharama kubwa ambazo wangelazimika kuzitumia
kufuata huduma hizo nje ya mkoa wao.
Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Matibabu na Ushauri wa Kitaalam Dk. Aifena Mramba
ambaye alimwakilisha Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Benrard Konga , akitoa maelezo ya
awali kwenye uzinduzi wa huduma hizo.
“ … Mfuko umetenda jambo jema sana na unapaswa kupongezwa hasa kwa kuona
umuhimu wa kusogeza huduma hizi karibu na wananchi wengi wenye mahitaji
kwa mfano mimi ni mjane hapa nilipo lakini mpango huu umeniwezesha kuwaona
hawa wataalam ambao kwa hali ya kawaida nisingewaona hivyo napongeza
Mfuko wa Serikali yetu inayoongozwa na Dk. Pombe John Magufuli,..” Alisema Bi.
Leah Ezekiel.
Akitoa maelezo ya awali Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa
Taifa wa Bima ya Afya , Dk. Aifena Mramba alisema kuwa kwa muda wa siku mbili
za zoezi hilo katika mikioa ya Kigoma na Geita, jumla ya wagonjwa 1,204,
wameonwa na kuhudumiwa na madaktari bingwa.
Alisema kuwa idadi hiyo imetoa taswira ya mahitaji ya wananchi katika huduma za
kibingwa jambo linalotoa hamasa kwa Mfuko kuangalia namna ya kuendesha
program hizo katika maeneo mengi zaidi.
Dk. Mramba akikabidhi Mashuka na Vifaa tiba kwa uongozi wa Mkoa wa Geita kwa ajili ya
matumizi ya zoezi la Madaktari Bingwa.
“…Kwa madaktari tuliowaleta, wametuhakikishia kuwa wako tayari kufanya kazi
kwa muda wowote ili wagonjwa wote waliofika kwa ajili ya mpango huo
wahudumiwe na mfano mzuri jana kuna madaktari waliofanya kazi hadi saa sita
usiku…” alisema Dk. Mramba.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita Selestine Gesimba, ambaye alimwakilisha Mkuu
wa Mkoa katika uzinduzi wa mpango huo, ameomba Mfuko wa Taifa wa Bima ya
Afya kuangalia namna ya kufanya huduma hizi kuwa endelevu kwa kuwa
zimeonyesha mafanikio makubwa katika kuwahudumia wananchi ambao uwezo
wao ni mdogo kufuata huduma mbali.
Aliviagiza vituo vya matibabu mkoani humo kuendelea kushirikiana na Mfuko wa
Taifa wa Bima ya Afya katika fursa mbalimbali zinazolenga kuboresha huduma
ikiwa ni pamoja na kutumia fursa ya mikopo ya vifaa tiba na ukarabati wa
majengo ili kuboresha huduma katika vituo vyao.
Aidha amewahimiza wananchi kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na
Mfuko wa Afya ya Jamii ili kujihakikishia upatikanaji wa kupata huduma kwa
kuchangia kabla ya kuugua na kuepukana na usumbufu wa kutafuta fedha za
matibabu wakati wanapougua.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita Selestine Gesimba akihutubia wananchi waliofika katika
uzinduzi huo.
Wananchi wenye uhitaji wa huduma za Kibingwa wakiwa kwenye mstari wa kuandikishwa.
Wananchi wakifuatalia hotuba ya uzinduzi wa zoezi hilo la madaktari Bingwa.
Wahudumu katika hospitali ya Mkoa wa Geita wakihesabu mashuka yaliyotolewa na NHIF.
No comments:
Post a Comment