HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, May 31, 2017

DC MBULU: AWAOMBA WANANCHI KUMUUNGA MKONO RAIS MAGUFULI

Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Mofuga amewataka wananchi wamuunge mkono Rais John Mafuguli, katika kuhakikisha anasimamia rasilimali za watanzania na kufanikisha maendeleo ya sekta mbalimbali.

Kwa mujibu wa Mofuga, wakati inakaribia miaka miwili ya utawala wa Rais Magufuli amefanikisha maendeleo mengi ambayo yangeweza kufanyika kwa kipindi cha utawala wamuda wa miaka 40.

Akizungumza na wananchi wa wilaya ya Mbulu, alisema miongoni mwa maendeleo hayo ni kuzindua na kuanza kwa ujenzi wa reli ya umeme, kuhamisha makao makuu ya nchi Dodoma mpango uliodumu tangu mwaka 1973 na kuanza maandalizi ya ujenzi wa barabara za ghorofa kwenye jiji la Dar es salaam.

Alisema amefanikisha kuongezeka kwa pato la Taifa kupitia ukusanyaji wa kodi kutoka sh850 bilioni kwa mwezi alipokuwa anaingia madarakani hadi kufikia sh1.2 trilioni kwa mwezi hivi sasa.

Alisema pia Rais Magufuli amefanikisha ununuzi wa ndege na kufufua shirika la ndege la ATCL, kutoa elimu bure kwa shule za msingi na sekondari jambo linaloongeza usajili wa wanafunzi mara mbili.

"Amegundua watumishi wenye vyeti feki 9,932 na watumishi hewa 19,706 ambao mishahara yao ilikuwa inatumiwa na watu wachache badala ya kupelekwa kwenye shughuli za maendeleo za wananchi ikiwemo elimu, afya na maji," alisema Mofuga.

Alisema Taifa lilishuhudia historia nyingine baada kupokea ripoti ya tume aliyounda ya kuchunguza mchanga wenye dhahabu (makinikia) yenye wajumbe nane wenye taaluma mbalimbali za uhandisi na kuchukua hatua stahiki mara baada ya kupokea.

"Kwenye taarifa hiyo ilibainika kuwa thamani ya madini yote kwenye makinikia ni makontena 277 yenye thamani ya sh829.4 bilioni kwa viwango vya wastani na viwango vya juu ni sh1.4 bilioni yaani dhahabu iliyokuwa kwenye makontena 277 ni sawa na lori mbili za tani saba ba pick up tani 1.5," alisema Mofuga.

Alisema Taifa lilikuwa linahitaji kiongozi aina ya Rais Magufuli kwa muda mrefu na kutokana na utekelezaji huo unaofanyika wananchi wanatakiwa kumuunga mkono ili aongeze jitihada za kuhakikisha Tanzania inafika kwenye nchi ya maziwa na asali.

Mmoja kati ya wakazi wa eneo hilo Yohana Amnaay alisema pamoja na jitihada hizo za Rais Magufuli pia mkuu huyo wa wilaya ya Mbulu Mofuga, amekuwa na utaratibu mzuri wa kutatua kero za jamii hasa migogoro ya ardhi kwa kukutana na wananchi.

"Kila alhamisi DC wetu amekuwa na utaratibu wa kukutana na wananchi hivyo kupitia nafasi hiyo jamii imekuwa inatatuliwa kero zake kuliko kukaa na kusubiri viongozi wakubwa wafike Mbulu ndiyo wananchi wafikishe malalamiko yao kwao," alisema Amnaay.'

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad