HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, February 22, 2017

SERIKALI KUONGEZA WATAALAMU SEKTA YA MAJI

Mkuu wa Chuo cha Maji Dkt.Shija Kazumba akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuhusu mkakati wa Chuo kuhakikisha Tanzania inakuwa na Mafundi Sanifu wa kutosha katika sekta ya maji ili kuendana na kasi ya Serikali kufikisha huduma ya maji kwa wananchi wote. Kulia ni Afisa Habari na Masoko wa chuo hicho Bw. George Karumuna.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano wa Chuo cha Maji na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam.

Fatma Salum-MAELEZO
Serikali imedhamiria kuzalisha wataalamu wa maji wa kutosha kukidhi mahitaji ya sasa na kuwafikishia wananchi wote maji safi na salama kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa kote nchini.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Chuo cha Maji cha Dar es Salaam Dkt. Shija Kazumba wakati wa mkutano na vyombo vya habari uliolenga kueleza mikakati ya chuo hicho ya kuzalisha wataalamu wenye sifa na weledi.
“Wanafunzi waliopo sasa ni 1849, kati yao 489 ni wanawake na dhamira yetu ni kuhakikisha  kuwa kuna mafundi sanifu wa kutosha kulingana na mahitaji ya sasa na ukuaji wa sekta ya maji”alisisitiza Dkt. Kazumba.
Alifafanua kuwa chuo hicho kimeanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kuwainua wanafunzi wa kike ili wajiunge katika masomo ya uhandisi wa maji, mafundi sanifu, upimaji wa ubora wa maji, umwagiliaji na hali ya hewa lengo likiwa ni kuchochea ukuaji wa sekta hiyo.
“Dhamira ya kuwainua wanafunzi wa kike inaonyesha nia ya Serikali kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika kukuza na kuendeleza sekta mbalimbali hapa nchini ikiwemo sekta ya maji”. Aliongeza Dkt. Kazumba
Pia alibainisha kuwa Serikali imewezesha kuwepo kwa maabara ya kisasa kwa ajili ya kupima ubora wa maji, kupima ubora wa mita na maabara ya kukata mabomba zote zikiwa na lengo la kuboresha hali ya upatikanaji wa maji safi na salama.
Dkt Kazumba alitoa rai kwa Halmashuri zote nchini kuajiri Mafundi Sanifu na Wahandisi wa Maji kwa ajili ya kuongeza tija katika sekta ya maji.
Alifafanua kuwa Mafundi Sanifu waliohitajika kwa kipindi cha mwaka 2013 ilikuwa ni 3000 na mwaka 2014 ilifikia 6000 na dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa kila mhandisi mmoja anakuwa na mafundi 5 wa kumsaidia kutekeleza majukumu yake.
Chuo cha Maji kilianzishwa mwaka 1974 kwa lengo la kuendeleza na kuzalisha wataalamu wa sekta ya maji kupitia mafunzo, ushauri na tafiti mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad