HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 11, 2017

Kaimu Mkurugenzi Mkuu NHIF azitaka hospitali zote nchini kutoa huduma bora kwa Wanachama wake

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga akiongozana na baadhi ya wakurugenzi wa Mfuko na uongozi wa Hospitali ya Kairuki walipotembelea maeneo mbalimbali ya hospitalini hapo kuangalia huduma zinazotolewa kwa wanachama wa Mfuko. Pichani akimjulia hali mwanachama wa Mfuko aliyelazwa hospitalini hapo.

Na Grace Michael

KAIMU Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bw. Bernard Konga amezitaka Hospitali zote nchini zinazohudumia wanachama wake kuhakikisha zinatoa huduma bora na zinazostahili kwa wanachama ikizingatiwa ukweli kwamba wamekwishazilipia huduma hizo kabla ya kuugua.

Aidha amewahakikishia wanachama wa Mfuko kwamba, Mfuko umejipanga kuwahudumia na kutatua kero wanazokabiliana nazo wakati wa kupata huduma ili wajivunie huduma walizolipia.

Bw. Konga amesema hayo wakati alipofanya ziara ya kujionea namna wanachama wa Mfuko wanavyohudumiwa katika Hospitali ya Kairuki mjini Dar es Salaam ambapo mbali na kuona huduma pia alipata fursa ya kuzungumza na wanachama waliofika hospitalini hapo kupata huduma.
Bw. Konga akiwasikiliza wanachama wa Mfuko waliokuwa wakipata huduma za matibabu hospitalini hapo.

Akizungumza na wanachama katika Hospitali ya Kairuki, Bw. Konga alisema kuwa ameamua kuanza ziara ya kutembelea hospitali zote ili kukutana na wanachama, kusikiliza kero zao pamoja na kuzungumza na watoa huduma kwa lengo la kutatua matatizo yaliyopo na kujenga uhusiano bora.

“Nimeamua kuanza rasmi ziara hizi za kikazi kuwaona moja kwa moja wanachama wanahudumiwa ili nizungumze nao na kupata maoni kutoka kwao…wanachama kwangu ndio kipaumbele cha kwanza kwa kuwa ndio wametupa dhamana ya kuwahudumia na kukaa na fedha zao hivyo binafsi sitakubali kuona mwanachama akipata huduma hafifu”. Alisema Bw. Konga.

Alisema kuwa kitendo cha kutoka na kusikiliza wanachama kitasaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma lakini pia kukutana uso kwa uso na wananchi ambao Mfuko unawahudumia.
Wakiendelea kupata maelezo ya huduma hospitalini hapo.

Wakizungumza mbele ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu huyo baadhi ya wanachama waliokuwa wakipata huduma hospitalini hapo, kwanza wameupongeza Mfuko kwa hatua hiyo ya kuamua kutoka nje kwa lengo la kukagua huduma lakini pia kwa maboresho mbalimbali ambayo yamefanywa na Mfuko.

“Hii kazi ambayo umeianza Mkurugenzi Mkuu ni nzuri sana na tunaomba pia hata vituo vya chini kwa maana ya Zahanati navyo vitembelewe ili kuwekewa utaratibu mzuri zaidi…matatizo bado yapo lakini kwa kiasi kikubwa mmejitahidi sana kuyatatua,” walisema wanachama hao.

Kwa upande wa Mwanachama wa Mfuko ambaye anahudumiwa na Mfuko chini ya Fao la Wastaafu Injinia Emmanuel Olekambainei ambaye alifika hospitalini hapo kwa ajili ya kupata huduma za macho, naye aliupongeza Mfuko na kumtaka Kaimu Mkurugenzi Mkuu kuangalia zaidi huduma ambazo haziko katika kitita cha mafao.
Bw. Konga akipata maelezo ya namna wagonjwa wanavyopokelewa.

Aidha Injinia Olekambainei alisema kuwa huduma za afya hususan zinazotolewa na Mfuko zimeboreshwa na hasa katika kipindi hiki cha Serikali ya awamu ya tano.

“Nawapongeza kwa kweli maana kuna mabadiliko makubwa na inatokana na kasi ya Serikali yetu hivyo hongereni sana maana mimi mwenyewe napata huduma hapa kwa mwamvuli wa ustaafu chini ya NHIF,” amesema Bw. Olekambaini.

Akizungumza na Uongozi wa Hospitali ya Kairuki,Bw. Konga alisema kuwa ni muda muafaka kwa Mfuko kushirikiana kwa karibu na watoa huduma kwa lengo la kutoa huduma bora kwa wanachama wa Mfuko.

Kwa upande wa Uongozi wa Hospitali ya Kairuki ulioongozwa na Mkurugenzi Mkuu Dr. Asser Mchomvu, alisema kuwa hawana matatizo na uhusiano kati yao na Mfuko kwa kuwa wanatambua mchango katika kuboresha huduma zao.
Wakipata maelezo kutoka katika chumba cha kuchakata madai ya huduma zilizotolewa kwa wanachama.

“Tuwe wazi kuwa bila NHIF hatuwezi kujiendesha hata siku moja na wagonjwa tunaowahudumia hapa zaidi ya asilimia 90 ni wanachama wa NHIF hivyo tunao wajibu wa kuhakikisha kwamba Mfuko hauyumbi kwa namna yoyote vile vile kwetu wanachama wa NHIF ndio wateja wetu wakubwa hivyo tunawathamini na kuwaheshimu sana,” alisema.

Alisema kuwa changamoto za kiutendaji kati yao na Mfuko zikiwemo za bei za huduma, mifumo na ulipaji wa madai wataendelea kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haziwakwamishi kutoa huduma kwa wanachama.

Akihitimisha ziara hiyo Bw. Konga alitoa wito kwa wanachama wote kuhakikisha wanatoa taarifa wakati wowote wanapokutana na changamoto wakati wa kupata huduma za matibabu.
Meneja wa Idara ya Ukjaguzi wa Kairuki akitoa maelezo ya huduma mbele ya wanachama na uongozi wa NHIF.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad