Kocha wa Muda wa Azam Fc Iddy Cheche
Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.
Kikosi cha Azam kinatarajiwa kuingia kambini kesho kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wao wa ligi kuu ya Vodacom dhidi ya Simba utakaofanyika Januari 28 siku ya Jumamosi kwenye Uwanja wa Uhuru.
Akizungumzia maandalizi kuelekea mtanange huo, Kocha wa muda wa timu ya Azam Iddi Cheche amesema wamejianda vizuri kuelekea mchezo wao dhidi ya Simba ambao umekuwa wa ushindani sana kutoka kila timu kutaka matokeo mazuri mbele ya mwenzake.
Katika mchezo wa raundi ya kwanza Simba walifanikiwa kutoka na ushindi waq goli 1-0 lakini kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi mapema mwezi huu Azam waliweza kulipa kisasi kwa kuifunga goli 1-0.
Cheche ameweka wazi kuwa Simba ni timu kubwa na tunapokutana na timu kubwa basi lazima wachezaji wacheze kwa umakini ili wasifanye makosa na zaidi hakuna timu inayopenda kufungwa mara mbili mfululizo kwahiyo tunajua mbinu za kutumia ili kuweza kuondoka na ushindi.
“Kikubwa tutajituma kwa kila hali tupate matokeo mazuri mbele ya vinara hao wa ligi kuu, licha ya kuwa na matatizo makubwa katika safu ya ushambuliaji ambayo imekuwa haina umakini,” alisema Cheche.
Kwa sasa wachezaji wa Azam wamepewa mapumziko baada ya kumaliza mchezo wa Kombe la Shirikisho FA dhidi ya Cosmopolitan uliofanyika jana na Azam kutoka na ushindi wa goli 3-1.
No comments:
Post a Comment