HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 15, 2016

MADINI YA BILIONI 3 YAKAMATWA YAKITOROSHWA

Siku chache baada ya Rais John Magufuli kusema kuna utoroshaji mkubwa wa madini kupitia viwanja vya ndege vilivyopo migodini, Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) umekamata madini yenye thamani ya Sh3,353,421,381.4 yakitoroshwa katika viwanja vikubwa vya ndege na katika matukio 25 tofauti.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa TMAA, Mhandisi Dominic Rwekaza ameeleza hayo katika ripoti ya ukaguzi iliyofanywa na wakala huo mwaka 2015 akisema: “Katika kufuatilia usafirishaji wa madini nje ya nchi katika viwanja vikubwa tulikamata madini yanayotoroshwa yenye thamani ya Dola za Marekani 1,512,186.61 na mengine ya Sh34,670,794 katika matukio 25 tofauti.” 

Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari nchini hivi karibuni jijini, Rais Magufuli alisema pamoja na kwamba Tanzania ina utajiri mkubwa wa madini, kumekuwa na utoroshwaji wa madini kwa ndege zinazoruka kutoka kwenye baadhi ya migodi.

“Tuna dhahabu ambazo zinachimbwa, lakini utakuta watu wanasafirisha makontena ya mchanga unapelekwa kwenda kusafishwa na sisi ndiyo tunasindikiza na wananchi mpo mnashangilia,” alisema Rais Magufuli.

“Kwa sababu kule wanakwenda ku-separate (kutenganisha). Kwa nini tusijenge separation plant hapa tukatengeneza ajira hapa kwa Watanzania,” alihoji. 

Viwanja vya ndege migodini 
Hata hivyo, wakala huo umesema suala la migodi mikubwa kuwa na viwanja vya ndege kwa ajili ya kusafirishia madini haliepukiki kwa sababu za kiusalama.

Akifafanua ripoti ya ukaguzi wa madini ya mwaka 2015, Msemaji wa TMAA, Isambe Shiwa alisema licha ya kudhibiti utoroshwaji huo viwanja vya ndege vinatumika kusafirishia madini kutoka migodini moja kwa moja kwa sababu za kiusalama.

“Katika maeneo yote ya madini, kuna mawakala wa ukaguzi wa madini, wanashuhudia uzalishaji wa madini, hasa kwa dhahabu wana chukua mikuo (mche wa dhahabu) yake na kuileta kwenye maabara zetu ili ipimwe kujua kiasi cha dhahabu na fedha kisha wanakokotoa mrabaha kulingana na madini husika,” alisema.

“Ili kujua faida ya madini katika mgodi husika, huwa tunafanya ukaguzi yakinifu na kukokotoa kodi zinazotakiwa hasa kodi ya shirika. Kama kuna utata kwenye taarifa za mgodi kuhusu ununuzi wa vifaa na mitambo, tunakagua na kuweka wazi gharama zake kisha tunapeleka TRA kiasi kinachotakiwa kulipwa.”

“Kwa mfano ukiangalia bei ya madini ya dhahabu, kwa wastani gramu moja huuzwa Sh100,000, hivyo kilo moja huuzwa Sh1 bilioni.Ule mkuo mmoja una kilo 20 hadi 25. Unaweza kuviweka vile vipande kwenye mkoba ila ni vizito kubeba. Ukishazalisha hadi mikuo 20 ya dhahabu unabeba mabilioni ya fedha, utasafirishaje kwa gari?

“Kuna wakati pale mgodi wa Geita (GGM) kulikuwa na ndege iliyobeba dhahabu, kumbe tayari watu walishatoa taarifa nje kwa watu waliojitayarisha na silaha za kivita, wakaitungua ilipokuwa ikiruka. Bahati nzuri rubani aliimudu na kufanikiwa kuirudisha uwanjani.”

Alisema kutokana na matukio hayo, sasa wanasafirisha madini kwa helikopta ambayo ikichukua mzigo hupaa kwenda juu zaidi kisha kwenda Dar es Salaam ambako hukaguliwa tena kabla ya kwenda nje ya nchi.

“Kutokana na ukaguzi unaofanyika, naweza kusema hakuna madini wala mchanga unaosafirishwa kwa wizi kwenye migodi yote.Kwanza hii migodi inamilikiwa na wana hisa walioko ndani na nje ya nchi. Wao nao wanataka kupata taarifa za ukaguzi wetu ili wajue wanalipa kodi kiasi gani na wanapata nini,” alisema.

Akizungumzia sababu za madini ya tanzanite kuuzwa zaidi na Kenya, Afrika Kusini na India, Shiwa alisema ni kutokana na Sheria ya Madini ambayo hukata mrabaha wa asilimia tano ya madini hayo wakati sheria ya nchi hizo haina, hivyo kuvutia zaidi wasafirisha madini kupitia nchi hiyo.

“Baada ya kugundua udhaifu huo, kamishna wetu wa madini na ofisa mtendaji wetu mkuu walikwenda Kenya kuzungumza nao ili nao waweke mrabaha huo na kweli waliweka. Hivyo kwa miaka minne iliyopita madini hayo yamepungua sana Kenya,” alisema.

Alisema wamechukua pia hatua ya kuongeza thamani ya madini hayo kwa kuyakata baada ya kujenga viwanda mkoani Arusha hivyo kupunguza usafirishaji wa madini ghafi kupitia Kenya, Afrika Kusini na India.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad