HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, November 28, 2016

Bayport yatoa msaada wa kompyuta za Sh Milioni 500 kwa Serikali

Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga akikabidhi moja ya kompyuta zilizokabidhiwa na Taasisi yake kwa ajili ya serikali. Anayepokea ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
TAASISI ya Kifedha ya Bayport Financial Services inayojihusisha na mikopo imeipatia serikali msaada wa kompyuta 205 zenye thamani ya Sh Milioni 500 kwa ajili ya matumizi yao ya kiofisi, kwa kupitia Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga wa pili kutoka kushoto waliosimama, akipeana mkono na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala, Mheshimiwa Angellah Kairuki baada ya kukabidhiwa kompyuta 205 na Taasisi ya Bayport, akifuatiwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Laurean Ndumbaro na Kaimu Katibu Mkuu Bi Susan Mlawi.

Makabidhiano hayo yamefanyika jana jijini Dar es Salaam, ambapo kompyuta 125 zitabaki Makao Makuu ya Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kompyuta 80 zilizosalia zitagawanywa na Wizara yenyewe kwa kuangalia mahitaji ya ofisi zao.
Baadhi ya Wakuu wa Idara kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakifuatilia halfa ya makabidhiano ya kompyuta kutoka kwa Taasisi ya Bayport Financial Services.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga, alisema msaada wa kompyuta hizo zinatokana na kiu yao kubwa ya kushirikiana na serikali kuboresha utendaji kazi wa watumishi wa umma kwa ajili ya kufanikisha huduma bora kwa Watanzania.

Alisema taasisi yao ilipanga wamalize mwaka kwa kukabidhi kompyuta kwa ofisi za serikali, ikiwa ni mwendelezo wa kusherehekea miaka 10 ya huduma zao tangu Bayport ilipoanzishwa mwaka 2006 nchini Tanzania.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki katikati akizungumza katika hafla ya kukabidhiwa kompyuta kutoka kwa Bayport Financial Services leo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Katibu Mkuu Dk Laurean Ndumbaro na kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Bayport, John Mbaga.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala, Mheshimiwa Angellah Kairuki wa pili waliosimama mstari wa mbele, akifuatiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bi Susan Mlawi pamoja na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk Laurean Ndumbaro kulia kwa waziri wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa Bayport na baadhi ya wakuu wa Idara wa Ofisi ya Rais.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki, akizungumza katika halfa ya makabidhiano kompyuta 205 za aina mbalimbali kutoka kwa Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services yenye Makao yake Makuu jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa huduma kwa ofisi za serikali nchini Tanzania. Kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Bayport, John Mbaga.

“Tunakabidhi kompyuta hizi 240 kwa serikali huku tukijipa moyo kuwa zitatumiwa ipasavyo na watumishi wetu wa umma wanaotuhudumia katika majukumu yao na kuongeza ufanisi, hivyo Bayport itaendelea kushirikiana na serikali kwa nguvu zote.

“Sisi jukumu letu ni kushirikiana na serikali sambamba na kujitolea kwenye jamii kwa kusaidia mambo mbalimbali kwa ajili ya kuwakwamua wateja wetu na Watanzania kwa ujumla kwa kupitia sekta ya mikopo,” Alisema.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki, aliishukuru Bayport kwa kutekeleza ahadi yao ya msaada wa kompyuta kwenye wizara yao.

Alisema wamevutiwa na kompyuta hizo zilizotolewa kwa wakati muafaka, huku akisema zitarahisisha utoaji wa huduma bora kwa watumishi wa umma katika ofisi watakazopokea baada ya kufikishwa kwao.

“Tulipata taarifa kuwa wenzetu wa Bayport wanatuletea msaada huu ambao kwa hakika ni mkubwa na umekuja wakati muafaka na utawawezesha watumishi wetu kufanya kazi vizuri kwa kupata hivi vitendea kazi,” alisema.

Bayport ni taasisi inayotoa huduma za mikopo ya fedha kwa watumishi wa umma na wafanyakazi wa kampuni binafsi, huku pia ikitoa huduma za mikopo ya viwanja katika miradi yake ya Bagamoyo, Kigamboni, Kibaha na Kilwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad