HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 15, 2016

MKUU WA MKOA WA MOROGORO, STEPHEN KEBWE ATEMBELEA UPIMAJI NA UMIRIKISHAJI WA ARDHI KATIKA KIJIJI CHA DIHOMBO NA HEMBETI, MVOMERO.

Bw. Charles Charokiwa Msumari(katikati) Afisa Mifugo Msaidizi Mkuu wa Tume ya Mipango na Matumizi ya Ardhi akitoa ufafanuzi kwa Mkuu wa mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe alipotembelea kituo chao ambacho wanakitumia kukusanyia taarifa mbalimbali na shughuli zao
Baadhi ya wadau mbalimbali wakiendelea kufuatilia kwa makini maelezo.
Dr. Stephen Nindi(katikati) Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango na Matumizi ya Ardhi Tanzania akimuelezea jambo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe walipotembelea eneo la upimaji.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe akipongeza hatua ya upimaji wa ardhi na kuahidi kuendelea kutembelea kuona maendeleo
Bw. Ally Amri(kushoto) ambaye ni  Land Surveyor akitoa maelezo kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe namna zoezi la upimaji linavyofanyika.
 Christian Thomas(aliyevaa shati la blue) ambaye ni mwenyekiti wa kijiji akimwelezea Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe namna zoezi la upimaji wa Ardhi lilivyo wasaidia
 Viongozi wa Serikali na wadau mbalimbali wakiwa katika eneo la moja ya kijiji kuona jinsi shughuli za upimaji zinavyokwenda 
 Hiki ni  kifaa kiitwacho Real Time Kinematic (RTK) ni moja ya kifaa cha kisasa kinachotumika katika upimaji wa ardhi.

Mtaalam wa GIS Theonest Mlolewe akimuonesha Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mh. Stephen Kebwe (hayupo pichani) namna wanavyofanya kazi.
Picha zote na Fredy  Njeje/ Blogs za Mikoa



MKUU wa Mkoa wa Morogoro Dkt.Stephen Kebwe amesema  kazi ya upangaji wa matumizi bora ya ardhi kwa kiasi kikubwa itapunguza na  kuondoa migogoro mbalimbali ya ardhi inayotokea katika kijiji kwa kijiji,kata kwa kata au kitongoji kwa kitongoji  na kusisitiza kuwa Serikali haitashindwa kumchukulia hatua za kisheria mtu yeyote atakaekwamisha kazi ya  upimaji wa ardhi yenye lengo la upangaji wa matumizi bora ya ardhi.

Akizungumza  na wanakijiji wa kijiji cha Dihombo,Dkt.Kebwe alisema kazi hiyo itasimamiwa kikamilifu na kamati husika za ulinzi na usalama kutoka Wilayani,Kata hadi Mkoa kuhakikisha inafanikiwa. Alisema kazi hiyo inayofanywa ya upimaji wa ardhi itakuwa ndio muarobaini wa kuondoa migogoro inayojitokeza mara kwa mara ikiwemo ya Wakulima na Wafugaji katika mkoa huo.

Alisema kwa sasa wapimaji wa ardhi wanatumia vipimo vya kisasa zaidi ambavyo kwa kiasi kikubwa vipimo hivyo vitaweza kupima ardhi kwa kipindi kifupi na kila mtu kumiliki kipande cha eneo lake.

"Nakumbuka wakati wa kampeni mwaka jana,Rais Dkt.John Magufuli alihaidi wazi kuwa kipindi cha miaka 10 kutakuwa na upimaji katika maeneo yote ya nchi kwa utaratibu wa mpango mzuri na wa kisasa,kwa miaka mitano hii vijiji takribani 7500  vitapimwa kwa kupangwa kila halmashauri 25 ambapo kwa kila mwaka vitapimwa vijiji 1500,"alisema. Alisema kuwa zoezi la upimaji linaloendelea hivi sasa ni sehemu ya utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM)kwa wananchi katika kuondoa migogoro inayojitokeza.

"Kazi hii ya upimaji wa maeneo katika kuhakikisha kunampango bora wa matumizi ya ardhi ni mpango wa nchi,ambapo serikali imechangua Mkoa wa Morogoro kuwa wa Mfano katika upimaji wa ardhi ambapo utahusisha nchi nzima,"alisema Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango na Matumizi ya Ardhi(NLUPC),Dkt.Stephen Nindi alisema ofisi yake inafanya kazi na wadau mbalimbali wa masuala ya ardhi zikiwepo wizara pamoja na mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali ikiwemo Shirika la Kimataifa la Care,Shirika la Oxfam,Chama cha Wafugaji Tanzania,Chuo kikuu cha Ardhi pamoja na Tamisemi.

Dkt.Nindi alisema kwa sasa kazi ya ya upimaji inafanywa na vifaa maalum vya kisasa vijulikanavyo kwa jina la Real Time Kinematic ambavyo vinafanya kazi kwa urahisi zaidi,licha ya vifaa hivyo kwa sasa vipo viwili nanvyakukodisha. "Tunahitaji kuwa na vifaa hivi walau vitano ambavyo vitatuwezesha kupima kwa wakati na kukaimilisha zoezi hili kwa haraka na kifaa kimoja kinagharimu kiasi cha sh.milioni 80,"alisema Dkt Nindi

Naye Mratibu wa Programu ya Ufugaji Asili kutoka Shirika la Kimataifa la Care,Marcely Madubi alisema suala la ardhi ni moja ya masuala muhimu yanayozingatiwa na shirika lao katika mikakati yao ya kimataifa. Alisema wadau mbalimbali nchini wanatakiwa kujitokeza kwa wingi katika kuchangia suala hili la kuhakikisha upimaji wa ardhi unafanikiwa hususani katika kuchangia ununuzi wa vifaa vya teknolojia mpya ya upimaji(Real Time Kinematic)ili kuwezesha upimaji wa ardhi kwenda kwa haraka zaidi na kupunguza migogoro inayoendelea kujitokeza.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad