HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 30, 2016

Ujio wa Ndege mpya za Air Tanzania kuongeza ushindani katika utoaji wa huduma za anga nchini

Hivi karibuni Serikali imetangaza kununua ndege nne katika kipindi cha mwaka huu wa fedha kwa ajili ya Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL)  ili kuimarisha sekta ya usafiri wa anga hapa nchini zitakazogharimu Dola za Kimarekani milioni 46.

Serikali kwa kuanzia imetoa asilimia 40 ambazo ni sawa shilingi bilioni 39,937,939,200 kwa ajili ya ununuzi wa ndege mbili za awali .ambazo zimelipwa Kampuni ya Bombadier Inc ya nchini Canada.

Azma hiyo ya Serikali ya kununua ndege mpya inatokana na ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kutaka kufufua Shirika la Ndege Tanzania na kulipatia mtaji ili lianze upya kutoa huduma hiyo kwa Watanzania.

Ujio wa ndege hizo utaimarisha huduma za usafiri wa anga na kuongeza ushindani katika utoaji wa huduma za anga hapa nchini kati yake na kampuni binafsi za ndege zinazotoa huduma hiyo kwa sasa.
Mara baada ya ndege hizo kuwasili hapa nchini zitaanza kutoa huduma ya usafiri wa anga hapa nchini kabla ya kupanua wigo wake wa utoaji wa huduma katika ngazi  ya ukanda wa Afrika Mashariki na baadaye katika anga.nyingine za Kimataifa.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Profesa Makame Mbarawa (MB) aliwasilisha Bungeni Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha hivi karibuni alisema kuwa Shirika la ATCL  lina ndege moja aina ya Dash 8-Q300 na ndege ya kukodi aina ya CRJ 200.

“Kwa sasa ATCL  ina ndege moja na ndege nyingine ni ya kukodi  ambazo zinawezeshwa na Serikali kutoa huduma za usafiri wa anga kati ya Dar es salaam, Mwanza, Mtwara, Kigoma na  Moroni Comoro” alisema Profesa Mbarawa.

Aidha,  Prof. Mbarawa aliongeza kuwa Wizara yake kwa kushirikiana na kampuni ya ATCL  na wadau wengine imekwishaainisha ndege mbili zinazofaa kununuliwa ambazo zitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 78  na  baadaye ndege nyingine mbili kubwa zitakazokuwa na uwezo wa kubeba abiria 155 ambazo zitanunuliwa kwa kipindi cha mwaka huo fedha.

Mchakato wa ununuzi wa ndege hizo mbili ambazo zitanunuliwa katika awamu ya kwanza ulihusisha wawakilishi wa viwanda vya ndege vya Boeing ya Marekani, Airbus ya Ufaransa, Embraer ya Brazil  na Bombadier ya Canada.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani alisema kuwa ndege hizo ambazo zinatarajiwa kununuliwa zitatumia anga la Tanzania ambapo hivi sasa anga hilo linatumiwa na ndege zinazotoka nje ya Afrika, hivyo upatikanaji wa ndege hizo utasaidia kutoa fursa kutua kwenye anga za nchi jirani.

“Muda si mrefu tutapata ndege mbili mpya, mwakani tutaongeza nyingine mbili, Serikali imejipanga kufufua Shirika la Ndege na kubadilisha mfumo wa uendeshaji ili liweze kujiendesha lenyewe” alisema Mhandisi Ngonyani.

Kwa mujibu wa Msemaji wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, (Mawasiliano) William Budoya , amesema kuwa msukumo wa kununua ndege hizo ni jambo la muda mrefu kuanzia Serikali ya Awamu wa Nne 2005-2015,na katika kuendeleza utekelezaji wa juhudi hizo Serikali ya Awamu ya Tano imetoa msisitizo na kulipa  kipaumbele suala hilo.

Aidha, Afisa Mawasiliano huyo amesema kuwa ndege zitakazonunuliwa ni aina ya Bombadier kutoka kampuni ya Bombadier Inc ya nchini Canada.
Serikali ilichagua kampuni ya Bombadier Inc kwa sababu iliainisha mchanganuo wa biashara ambao ulishauri kuanza na ndege ndogo, kwa kuangalia soko la ndani baadaye ndege zinaweza kuongezwa kwa kuangalia soko la kimataifa.

Aliongeza kwa ndege hizo zinatarajia kufika nchini ifikapo mwezi Septemba mwaka huu, na kwa kuanzia zitaanza kutoa huduma kwa safari za ndani ya nchi.

Aidha alisema kuwa Serikali imemteua  mshauri mwelekezi ambaye ataweka manejimenti imara katika uendeshaji ikiwa ni pamoja na kuajiri wafanyakazi walio na weledi na wenye utayari wa kufanya kazi kwa ufanisi.
Shirika la ndege la Tanzania (ATC) lilianzishwa mwezi Machi, 1977 chini ya sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1969 na baada ya kuvunjwa kwa lililokuwa Shirika la ndege la Afrika Mashariki.

Katika kutekeleza sera ya  ubinafsishaji na ushirikishwaji wa sekta binafsi katika uendeshaji wa Mashirika ya Umma ya mwaka 2002,  Shirika la ndege la Tanzania (ATC) liliundwa upya huku Serikali ikimiliki   asilimia 49 ya hisa zake kwa Shirika la ndege la Afrika Kusini hatua ambayo  ilipelekea kuundwa upya kwa kampuni ya ndege Tanzania (ATCL).

Pamoja na kuwepo kwa kampuni ya ndege ya ATCL, kwa sasa kuna kampuni binafsi zinazojihusisha na huduma za usafiri wa anga nchini na nje ya nchi.Kampuni hizo ni Precision Air, Fastjet, Auric na Coastal Air.

Akizungumzia mpango wa Serikali wa kukabiliana na changamoto ambazo zimekuwa zikiikabili kampuni ya ATCL , Budoya alisema kuwa mshauri mwelekezi aliyeteuliwa na Serikali  atatayarisha mpango madhubuti wa kibiashara utakaoifanya kampuni ya ATCL kujiendesha kwa faida na kuweza kuteka soko la ndani na nje ya nchi.

Majukumu ya sekta ya uchukuzi yanasimamiwa Sera ya Taifa ya Uchukuzi ya mwaka (2003) na utekelezaji wake ambao unahusu usafiri na usafirishaji kwa njia ya anga, kusimamia viwanja vya ndege na usalama katika usafirishaji nchini.Na Jovina Bujulu, MAELEZO

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad