
JUMLA ya miradi 13 yenye thamani ya Zaidi ya shilingi milioni 1.2 inatarajiwa kuzinduliwa pamoja na kuwekwa mawe ya msingi na Mwenge wa uhuru utakapokimbizwa katika Halmashauri ya wilaya ya Mufindi mapema alhamisi ya tarehe 25 mwezi huu.
Taarifa ya Ofisi ya habari na mawasiliano ya halmashauri ya Mufindi kwa vyombo vya habari imefafanua kuwa, vyanzo vya fedha zilizotumika kukamilisha miradi hiyo vimegawanyika katika sehemu kuu nne, ambapo asilimia 10 ya fedha hizo ni kutoka serikali kuu, asilimia 12 ni Fedha za Halmashauri, wakati asilimia 13 ni fedha za wahisani huku wananchi wakichangia asilimia 65.
Taarifa hiyo imeendelea kubainisha kuwa miradi hiyo 13 imegawanyika katika vijiji vya Mtili, Lugolofu, Mabaoni, Idetelo, Lugongo na kata ya Kinyanambo huku miradi mikubwa Zaidi ni pamoja na mradi wa sakosi ya Faraja wenye gharama ya Zaidi ya sh milioni 478 utakaozinduliwa katika kata ya Kinyanambo sanjari na mradi wa msitu ulioghalim Zaidi ya Sh. Milioni 180 utakao kaguliwa katika kijiji cha Lugongo.
Aidha, Mwenge wa uhuru utakabidhiwa kwa Halmashauri ya wilaya ya Mufindi, katika hafla itakayo fanyika kwenye uwanja wa shule ya sekondari Kinyanambo majira ya saa mbili asubuhi, ukitokea Manispaa ya Iringa na badaye jioni utakesha katika kijiji cha Mabaoni Mgololo kata ya Makungu.
Mwenge wa uhuru uliasisiwa rasmi mnamo mwaka 1960 na hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, ukiwa na shabaha ya kuleta matumaini, upendo, heshima na kuchochea maendele katika jamii za kitanzania.

No comments:
Post a Comment