HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 11, 2014

Wataalamu Nishati na Madini watakiwa kuwa wabunifu

Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya Petrogas inayojihusisha na kutoa mafunzo kwa ajili ya uandaaji wa mapendekezo ya miradi pamoja na usimamizi wake yenye makazi yake jijini Dar es Salaam Bw. Greyson Kiondo akisisitiza jambo kwenye mafunzo yanayohusu uandaaji wa mapendekezo ya  miradi na usimamizi wake yaliyoshirikisha wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini yanayoendelea mjini Bagamoyo katika hoteli ya Stella Maris.
Msimamizi wa mradi unaohusika na kuwajengea uwezo wataalamu wa nishati na tasnia ya uziduaji (CADESE; Capacity Development in the Energy Sector & Extractive Industries) Bw. Paul Kiwele (kulia) akisisitiza jambo kwenye mafunzo hayo. Kushoto ni Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga.
Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga ( wa kwanza kulia mbele ), msimamizi wa mradi wa CADESE Bw. Paul Kiwele (katikati) na baadhi ya washiriki wakiendelea kufuatilia mada iliyokuwa inawasilishwa na mtaalamu mwelekezi Bw. Tom Mitro kutoka Petrogas (hayupo pichani).
Mtaaalamu kutoka Petrogas Bw. Tom Mitro akiwasilisha mada juu ya uandaaji wa mapendekeo ya miradi katika semina hiyo mbele ya washiriki (hawapo pichani).
Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga (kushoto) akisoma hotuba ya ufunguzi kwa niaba ya Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli Mhandisi Hosea Mbise kwenye mafunzo hayo. Kulia ni msimamizi wa mradi wa CADESE Bw. Paul Kiwele.

Na Greyson Mwase, Bagamoyo
Waatalamu   kutoka katika Sekta za Nishati na Madini nchini wametakiwa kuwa wabunifu katika maandalizi na usimamizi wa miradi ili sekta hizo  ziwe na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Wito  huo umetolewa na  Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga  kwa niaba ya  Kamishna wa Nishati na Maendeleo  ya Petroli Mhandisi  Hosea Mbise alipokuwa akifungua mafunzo  ya uandaaji wa mapendekezo ya miradi, sera na mbinu za usimamizi wa miradi yaliyoshirikisha wataalamu kutoka  Wizara ya Nishati na Madini,  Shirika la Umeme Nchini, (TANESCO), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA)  na Kampuni ya Uendelezaji  wa Jotoardhi (TDGC) yanayoendelea mjini Bagamoyo.


Mafunzo haya yanatolewa na mtaalamu mwelekezi ambaye ni kampuni ya Petrogas yenye makazi  yake jijini Dar es Salaam.

Mhandisi Luoga alisema kuwa  Serikali imekuwa ikikumbana na changamoto  mbalimbali  katika usimamizi wa miradi yake ya maendeleo, hivyo ni  vyema wataalamu hao mara baada ya kumaliza mafunzo hayo wakawa wabunifu kiasi cha kuweza kuandaa mapendekezo ya miradi yanayotekelezeka, huku yakiendana na  kiasi cha bajeti  iliyotengwa.

 “ Kama  Wizara  tuna kazi  nyingi zinazotakiwa kutekelezwa ambazo zinahitaji uandaaji  makini wa mapendezo ya miradi ( “project proposals”)  ambazo zinahitaji utaalamu wa hali ya juu kuanzia  uanzilishi wa miradi, utekelezaji wake na tathmini yake kulingana na kiasi cha  fedha kilichotengwa, hivyo  lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo wataalamu wa sekta za nishati na madini.” Alisema Mhandisi Luoga.

Wakati huo huo msimamizi wa mradi unaohusika na   kuwajengea  uwezo wataalamu wa nishati na tasnia  ya uziduaji (CADESE; Capacity  Development  in the Energy Sector & Extractive Industries) Bw. Paul Kiwele alisema kuwa lengo la  mafunzo hayo ni kuwajengea  uwezo wataalamu  kutoka sekta za nishati  na madini  katika uandaaji wa mapendekezo ya miradi mbalimbali ( project proposals) na sera na hivyo  kuepusha  gharama ya kutumia wataalamu kutoka nje na kukuza umiliki.

Alisema kuwa  mafunzo hayo  yatakayochukua wiki tatu  yatashirikisha washiriki  60 ambapo kila kundi la washiriki 20 litajifunza kwa muda wa wiki moja, na kuongeza kuwa  kundi la kwanza litajifunza juu  ya uandaaji wa  mapendekezo ya miradi na kufanya  tathmini yake  ( project proposals preparations and  evaluations ), kundi la pili litajifunza juu ya uandaaji wa sera na kundi la tatu litajifunza juu ya usimamizi wa miradi.

Akizungumzia  uanzishwaji wa mradi wa CADESE,  Bw. Kiwele alisema kuwa mradi huo  ulizinduliwa mwaka huu  na  Katibu Mkuu wa Wizara  ya Nishati na Madini Bw.  Eliakim Maswi kwa kushirikiana na  Mkurugenzi Mkazi wa UNDP Bw. Phillipe Poinsot.

Alisema mradi huu unaofadhiliwa na  Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia  Maendeleo (UNDP) na  unatekelezwa na Wizara  ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na wadau wengine kama  vile Wakala wa Nishati  Vijijini (REA), Ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG),  Taasisi ya  Uogozi na  Taasisi  ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad