Tuesday, February 13, 2024

KONGAMANO LA WATAALAMU WA VYUO VIKUU TANZANIA NA FINLAND LAFANYIKA UDSM

NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

MAENDELEO yanayoongezeka katika teknolojia ya kijografia na teknolojia ya habari yanahitaji aina mpya ya wahitimu ambao wanauwezo na walio na ujuzi wa lazima wa kushughulikia changamoto mbalimbali za jamii kupitia teknolojia na uvumbuzi.

Ameyasema hayo leo Februari 13,2024 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye wakati wa Kongamano la Wataalamu wa Vyuo Vikuu Tanzania na Finland lililofanyika katika Ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam.

Amesema kuwa mradi wa GeoICT4e ni alama muhimu ambayo inajitahidi kuimarisha uwezo wa vyuo vikuu vya Tanzania katika elimu ya jeografia na teknolojia ya habari.

"Muhimu katika mabadiliko yetu ya elimu na dhana ya multicompetence learning( MCL) huwapa wanafunzi ujuzi wa vitendo katka teknolojia za kijografia digitali lakini pia kukuza uwezo wao wa kushughulikia matatizo ya ulimwengu wa kweli kwa ushirikiano, na kukuza imani ya kitaaluma na uelewa wa kina wa maswala ya jamii". Amesema Prof. Anangisye.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Tehema Dkt. Nkundwe Mwasaga amesema kuwa kazi ya serikali  ni kuwatengenezea mazingira mazuri vijana katika kuhakikisha wanapata fursa katika  mapinduzi ya kidijiti.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo kikuu Ardhi Prof. Evaristo Liwa amesema mashirikiano na vyuo vikuu vya Finland utaleta manufaa kwani watafiti wa Finland wameshatafiti juu ya Tanzania hivyo ni wakati muafaka kwa watafiki wa Tanzania kwenda kutafiti huko Finland.

Aidha Mratibu wa GeoICT4e  Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam Dkt . Mercy Mbise amesema mashirikiano na  vyuo vikuu vya Finland utaleta tija hususani kwa chuo kikuu cha Dar es salaam  katika kuhakikisha wanafunzi wanafundishwa ujuzi wa kidijiti utakaowafanya kwenda kufanya kazi huko duniani.








No comments:

Post a Comment