HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 20, 2023

Serikali ya Zanzibar yaiunga mkono Airpay kuboresha malipo kwa njia ya kidigital

NA MWANDISHI WETU, ZANZIBAR

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeiunga mkono Kampuni ya Airpay Tanzania katika adhma yake ya kutoa huduma za uhakika za malipo ya fedha kwa njia ya kidigitali kwa kuahidi kushirikiana nao katika kuhakikisha jambo hilo linafanikiwa na linaanza kwa muda uliyopangwa.

Aidha imesema zaidi ya asilimia 70 ya wajasirimali waliopo Zanzibar bado hawajatambulika rasmi katika mifumo ya Serikali hivyo kampuni hiyo ya Airpay imeonyesha utayari wao wa kushirikiana na Serikali kuwezesha kundi hilo kutambulika.

Hayo yote yamebainishwa leo visiwani Zanzibar na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji Mudrick Ramadhani Soraga wakati Benki Kuu ya Tanzania Ofisi ya Zanzibar ikiikabidhi leseni Kampuni ya Airpay Tanzania tukio lililoenda sambamba na ufunguaji rasmi wa ofisi ya kampuni hiyo iliyopo Mlandege, Zanzibar.

Soraga amesema serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa kampuni hiyo kwa sababu imekuja na teknolojia ya hali ya juu ambayo itakuja kufanya mageuzi makubwa ya Tehema ndani ya nchi ambayo siyo tu yatawanufaisha wajasirimali wadogo bali na benki na watoaji wa huduma wengine wa malipo.

“Hii ni kampuni ambayo ina uzoefu na biashara kwa zaidi ya miaka 12, kikubwa kama Serikali tutawapa ushirikiano wa hali ya juu ili zile huduma ziweze kupatikana kwa wananchi, tumekubaliana kwamba ni muhimu wakabaki katika misingi yao hasa kuwaangalia wajasiriamali wadogo, wa kati na hatimaye wale wakubwa,” amesema

Aidha amesema Airay Tanzania ni kampuni ya kwanza kuweka makao yake makuu visiwani Zanzibar ikiwa ni moja ya mkakati wa Serikali katika kuvutia wawekezaji katika masuala ya Tehama na masuala mazima ya mifumo.

“Nawapongeza Airpay kwa kuamua kufanya maamuzi mazito ya kuwekeza Zanzibar na kuifungua kama kitovu cha uwekezaji wa mifumo ya Tehama na sehemu ambayo itajulikana duniani kwamba inakaribisha kampuni mbalimbali ya Tehama,” amesema

Naye Kamishna wa Idara ya Mashirikiano baina ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPP), Dk. Bili Mrima Kiwia amesema wanaiunga mkono kampuni hiyo kwa sababu itaongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za malipo kwa njia ya mtandao kwa wananchi.

“Kampuni hii inajihusisha na mifumo mbalimbali ya malipo na wapo kuangalia ni kwa namna gani wataweza kuunganisha mifumo iliyopo kwa lengo la kurahisisha ufanyaji wa biashara ili kuweza kuwasaidia wajasiriamali wadogo wadogo waliopo Zanzibar kuweza kufanya biashara pamoja na kukopesheka,” amesema

Meneja Uchumi Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ofisi ya Zanzibar, Moto Lugobi amesema wametoa leseni kwa kampuni hiyo baada ya kujiridhisha kuwa itatoa huduma hiyo kwa misngi waliyokubaliana.

Kwa upande wake Mwanzilishi wa Kampuni ya Airpay, Kunal Jhunjhunwala amesema mtazamo wa kampuni hiyo ni kutoa huduma bora na za uhakika kwa Zanzibar na Tanzania bara kwa ujumla.

“Zanzibar ni mdau sahihi wa kushirikiana naye hasa katika kulasimisha mifumo ya kidigitali, tumevutiwa na serikali hii kwa sababu haichelewi kufanya maamuzi, tumejipanga kuhakikisha tunatoa huduma bora kwa njia ya kidigitali, hivyo watanzania walipo Visiwani Zanzibar na Bara watupokee kwani watapata huduma nzuri kwa wakati,” amesema Jhunjhunwala

Naye Makamu Rais na Meneja Mikakati wa Kampuni hiyo, Mihayo Wilmore amesema leseni hiyo mpya inaipa kampuni uwezo wa kufanya kazi ndani ya mfumo ikolojia wa fedha wa Tanzania, na hivyo kuimarisha uwepo wake barani Afrika.









No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad