HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, November 15, 2020

MATUKIO MAKUBWA MANNE YA TAASISI YA DORIS MOLLEL KUELEKEA SIKU YA MTOTO NJITI DUNIANI...

 *Watoto zaidi ya 150 waliozaliwa kabla ya wakati wafanyiwa vipimo kuchunguza afya zao

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

TAASISI ya Doris Mollel Foundation ambayo inahusika na kusaidia watoto wanaozaliwa kabla(Watoto Njiti), imejipanga kufanya matukio makubwa manne kuelekea siku ya Mtoto Njiti Duniani.

Miongoni mwa matukio hayo limo la kuandaa kliniki maalum ambapo akina mama zaidi ya 150 wamepeleka watoto wao wamezaliwa kabla ya wakati kwa ajili ya kuangalia maendeleo ya afya na makuzi yao kama yako sawa na watoto wengine ambapo madaktari bingwa wa watoto wametoa huduma kwa watoto hao.

Akizungumza na Michuzi Blog na Michuzi TV jijini Dar es Salaam wakati wa shughuli za kufuatilia afya za watoto waliozaliwa kabla ya wakati , Muasisi na Mkurugenzi wa Doris Mollel Foundation Doris Mollel amefafanua wamekutana hapo kuelekea siku ya mtoto njiti itafanyika Novemba 17.

Hivyo wameandaa matukio manne muhimu, ambapo tukio la kwanza ni  kuingia makubaliano ya kufanya kazi pamoja na Mtandao wa Jamii Forum kwa ajili ya kupeleka ujumbe wao kwa jamii hasa wale wanaotumia mitandao.

"Tukio la pili,taasisi yetu leo imefanya zoezi la kuangalia makuzi ya watoto wamezaliwa kabla ya wakati, na kazi iliyofanyika ni kuangalia je mtoto huyu anaongea kama watoto wengine wenye umri husika?Je anakuwa kama watoto wengine, uelekeo wake ukoje anaonesha dalili yoyote ya ulemavu au yuko kawaida, kwa hiyo hayo yote tunafanya kama taasisi.

"Kitu kingine ambacho tutakifanya kwenye tarehe hiyo 17 ambayo ni siku ya mtoto njiti duniani, tutafanya kazi kubwa ya kuwasha taa za zambarau kwenye jengo la wodi ya wazazi ya watoto njiti wapo na hasa wale ambao wanahudumiwa na huduma ya ngozi kwa ngozi na tutawasha taa hizo kwa kuamanisha tunaelimisha jamii kuhusu watoto njiti.

"Na tutawakumbuka wale watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati milioni 15 kwa kila mwaka pamoja na wale wanaopoteza maisha kwa kuzaliwa kabla ya wakati.Siku hiyo pia itakuwa wasaaa wa kuzunguma yale ambayo wameyafanya kwa miaka mitano sasa toka tumeanza kumzungumzia mtoto aliyezaliwa kabla ya wakati.

"Na tukio la nne ambalo Taasisi tutalifanya ni kukusanya fedha kwa ajili ya kusaidia Hospitali ya Wilaya ya Amana kwa kuwapatia vifaa tiba katika wodi yao ya watoto njiti. Kwa hiyo zote hizo ni jitihada za kuendelea kuimarisha huduma ya afya kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati na sisi kama wadau katika sekta ya afya tunafanya kazi kubwa ya kuisaidia Serikali kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka mitano hasa vinavyotokana na kuzaliwa kabla ya wakati,"amesema Mollel.

Kuhusu tukio la kufanya uchunguzi wa watoto waliozaliwa kabla ya wakati ambalo wamelifanya leo, Mollel amesema wameshirikiana na na Hospitali ya Taifa Muhimbili  ambao wao wamepeleka  madaktari kwa ajili ya kuhudumia watoto waliozaliwa kabla ya wakati na akina mama.

Pia wameshirikiana na Hospitali ya Aga Khan na kwa hiyo kazi kubwa inayofanyika ni wao kuendelea kushirikiana na vitengo vinavyofanya kazi kwenye wodi za watoto njiti na ndio maana katika tukio hilo wauguzi kutoka Hospitali za Temeke, Amana na Mwananyamala wameshiriki.

"Hivyo tunashukuru viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo na akina mama zaidi ya 150 wamejitokeza kujua maendeleo ya watoto wao ambao wamezaliwa kabla ya wakati .Ni kitu ambacho tumekifanya kwa mara ya kwanzana lakini mapokeo yamekuwa makubwa.

"Na matarajio yetu tutaendelea kufanya na miaka mingine inayokuja, na tutakwenda na mikoa mingine kwa kushirikiana na mikoa husika,"amesema.

Kuhusu ujumbe wake kwa Watanzania kuelekea siku ya Mtoto Njiti Duniani, Mollel ameishauri jamii kuendelea kuwa pamoja kwa ajili ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati , tujali kesho yao."Tunapojali hiyo kesho tutaangalia pia na wale baba na mama ambao wanatarajia kupata mtoto ambao ni vema wakafa na uelewa kuhusu watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

"Hivyo ni kazi kubwa kwa vyombo vya habari kuhakikisha ujumbe unaokwenda kwa jamii kuhusu watoto wanalozaliwa kabla ya wakati unakuwa sahihi,"amesema Mollel na kuhusu muako kwa wababa ambao wana watoto njiti amesema bado muamko sio mkubwa na hivyo wanawake ndio ambao wanaonekana kufuatilia zaidi maendeleo ya watoto wao.

"Niendelee kutoa mwito kwa wababa ambao wanawatoto njiti kushiriki kikamilifu katika maelezi , hata hivyo kuna dalili nzuri maana leo hapa tumeona akina baba wengi leo wamekuja na watoto wao kujua maendeleo ya watoto wao,"amesema.

Madakatari kutoka hospitali mbalimbali za Jijini Dar es Salaam wakiendelea na kliniki maalum ambapo akina mama zaidi ya 150 wamepeleka watoto wao wamezaliwa kabla ya wakati kwa ajili ya kuangalia maendeleo ya afya na makuzi yao kama yako sawa na watoto wengine iliyoandaliwa na Dorris Mollel Foundation na kufanyika katika ukumbi wa Don Bosco jijini Dar es Salaam.Watoto Njiti wakisubilia kupewa huduma na Madakatari  kutoka Muhimbili na Aga Khan wakati wa zoezi la kutoa huduma za kiafya kwa watoto njiti iliyoandaliwa na Dorris Mollel Foundation na kufanyika katika ukumbi wa Don Bosco jijini Dar es Salaam.Mkurugenzi na Mhasisi wa Doris Mollel Foundation, Doris Mollel akizungumza na wakina mama waliofika na watoto wao kwenye kliniki maalum ambapo akina mama zaidi ya 150 wamepeleka watoto wao wamezaliwa kabla ya wakati kwa ajili ya kuangalia maendeleo ya afya na makuzi yao kama yako sawa na watoto wengine  iliyoandaliwa na Dorris Mollel Foundation na kufanyika katika ukumbi wa Don Bosco jijini Dar es Salaam.Mkurugenzi na Mhasisi wa Doris Mollel Foundation, Doris Mollel akizungumza na waandishi wa  habari kuhusu taasisi hiyo ilivyoweza kuandaa kliniki maalum ambapo akina mama zaidi ya 150 wamepeleka watoto wao wamezaliwa kabla ya wakati kwa ajili ya kuangalia maendeleo ya afya na makuzi yao kama yako sawa na watoto wengine ambapo madaktari bingwa wa watoto wametoa huduma kwa watoto hao lililofanyika ukumbi wa Don Bosco Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad