HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, July 17, 2019

MAKALA-LINDI YANG'ARA MATOKEO KIDATO CHA SITA

*Mwanafunzi wake aibuka nafasi ya saba Kitaifa masomo ya lugha na sanaa
*Yaupandisha mkoa kutoka nafasi ya pili hadi nafasi ya kwanza Kitaifa
*Mkuu wa Mkoa wa Lindi atuma salamu kwa mikoa mingine ijipange

WAHENGA walisema ‘penye nia pana njia’ usemi huu umejidhirisha katika matokeo ya kidato cha sita kwa mwaka huu wa 2019, baada ya shule zote Mkoani Lindi zikiongozwa na shule ya Sekondari ya Nyangao kufanya vizuri katika matokeo hayo na kuufanya mkoa kushika nafasi ya kwanza katika mpangilio wa ubora wa ufaulu nchini.

Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna aliyetarajia kuona mkoa wa Lindi ukiibuka kidedea kwani kwa miaka mingi mikoa ya kusini ukiwemo Lindi ilisifika kwa kuwa nyuma kielimu kutokana na matokeo yasiyoridhisha yaliyokuwa yanapatikana.

Matokeo duni kielemu yalichangia kudorora kwa maendeleo ya mikoa hiyo kwa kiasi kikubwa. 

Jitihada mbalimbali zilizofanyika kwa ushirikiano wa Serikali, wazazi na wadau wa maendeleo kuhakikisha mikoa hiyo inaondoka katika kundi la kuongozwa zimezaa matunda kufuatia matokeo mazuri.

Hamasa kubwa inajengwa kwa wazazi na walezi kutambua umuhimu wa elimu kwa watoto wao kwa ajili ya faida yao na Taifa kwa ujumla. Kampeni kuhusu kipaumbele cha elimu ndio ukombozi katika kupambana na umaskini imeleta matokeo chanya mkoani Lindi. 

Mara baada ya uhuru Hayati Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere alihakikisha kuwa, Watanganyika wanakuwa na elimu ili waweze kujikomboa kutoka utumwa wa wakoloni na kujiongoza katika kujieletea maendeleo kwenye maisha yao. 

Akizungumzia kuhusu matokeo hayo Mkuu wa mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi alisema kuwepo kwa dhamira ya dhati iliyooneshwa na viongozi wa Serikali katika ngazi mbalimbali, wanasiasa na wananchi wa mkoa wa Lindi ili kuboresha na kuinua kiwango cha ufaulu imeanza kuonekana, ambapo kwa sasa mkoa unaongoza matokeo kidato cha sita na kufaulisha wanafunzi wote.

Alisema anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwezesha mkoa huo kufanya vizuri katika nyanja mbalimbali za kimaendeleo ikiwe kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu. Hali hiyo imetokana na mikakati mbalimbali iliyofanywa kati ya walimu, wanafunzi na Serikali.

Alisema hatua ya kwanza waliyoichukua ni kutafuta sababu za mkoa kutofanya vizuri kielimu, baada ya kuzibaini waliweka mikakati ya kutatua changamoto hizo kwa kusimamia mahudhurio ya wanafunzi kwa sababu kulikuwa na utoro  pia ukaguzi kwa walimu pamoja kuandaa majaribio ya mara kwa mara.

“Pia tulikuwa tunafanya mikutano ya kujadili na kuweka mikakati ya kuinua kiwango cha elimu katika mkoa wa Lindi kwa ushirikiano baina ya Serikali na wadau wa masuala ya elimu. Tulikubaliana kufanya ziara za mara kwa mara mashuleni pamoja na kuanzisha vituo kwa ajili ya wanafunzi wanaojiandaa na mitihani.”

Kiongozi huyo aliongeza kuwa hakuna mkoa uliondikiwa kuwa wa mwisho, waliamua kufanya jitihada mbalimbali ili kuuwezesha mkoa wao kusonga mbele kimaendeleo na wameanza kuyaona mafanikio, hivyo mikoa mingine inayodhani kuwa itakuwa ya kwanza kila wakati ijipange. 

Alisema kuwa katika mkoa wao kulikuwa na shule ya Sekondari ya Nyangao ambayo ilikuwa imeshapotea katika ramani, lakini kutokana na jitihada mbalimbali zilizofanywa na wadau wa elimu shule hiyo imeibuka na kuwa ya kwanza Kitaifa. “Hili ni jambo la faraja.”

“Niwapongeze walimu wote na wanafunzi kwani shule zote tisa za sekondari za kidato cha tano na sita mkoani hapa zimefanya vizuri katika matokeo ya kidato cha sita na kuufanya mkoa kuongoza mikoa yote. katika shule hizo nane ni za Serikali na moja inamilikiwa na mtu binafsi.”

Shule zilizofanya vizuri

Shule ya Sekondari ya Nyangao iliyopo Halmashauri ya wilaya ya Lindi imeshika nafasi ya kwanza Kitaifa kati ya shule 134 zenye wanafunzi chini ya 40, ambapo kati ya wanafunzi 25 waliofanya mtihani wa kumaliza kidato cha sita wanafunzi 22 walipata daraja la kwanza huku watatu waliosalia walipata daraja la pili.

Mwanafunzi wa shule hiyo ya sekondari ya Nyangao, Karimu Kassimu Muhibu (HKL) ameibuka katika namba saba kati ya wanafunzi kumi bora waliofanya vizuri Kitaifa katika masomo ya lugha na sanaa. 

Mbali na shule ya Sekondari ya Nyangao kupata matokeo hayo, shule zingine za sekondari za mkoa wa Lindi zilizopata matokeo mazuri ni shule ya kutwa ya Nachingwea iliyokuwa na watahiniwa 64 kati yake 49 walipata daraja la kwanza na waliosalia 15 walipata daraja la pili.

Shule ya sekondari ya kutwa ya Liwale kati ya wafunzi 186 waliofanya mtihani wanafunzi 43 walipata daraja la kwanza, 121 walipata daraja la pili na wanafunzi 22 walipata daraja la tatu.

Shule ya sekondari ya Mbekenyera iliyoko wilayani Ruangwa ambayo kati ya wanafunzi 98 waliofanya mtihani huo, wanafunzi 37 walipata daraja la kwanza, 56 walipata daraja la pili huku wengine watano waliosalia walipata daraja la tatu.

Shule ya sekondari ya Kilwa ambayo ilikuwa na jumla ya wanafunzi 103 walioifanya mtihani huo, wanafunzi sita walipata daraja la kwanza, 76 walipata daraja la pili huku weingine 21 wakipata daraja la tatu.

Ni dhahiri kwamba matokeo hayo ni ishara nzuri inayoashiria kuwepo kwa mwamko wa kutosha na kukubali mabadiliko makubwa ya kielimu miongoni mwa wananchi wa mkoa wa Lindi 

Inatarajiwa kuwa hatua hizo zitachangia kuongezeka kwa wasomi katika jamii za wakazi wa mkoa huo, ambao kwa vyovyote vile wanafunzi hawa watakuwa mabalozi wazuri wa kuhamasisha umuhimu wa elimu kwa wenzao ambao bado wanasoma katika ngazi mbalimbali zikiwemo shule za msingi.

Wanafunzi waliofanya vizuri katika matokeo ya kidato cha sita wanatarajiwa hapo baadae kusaidia mkoa wa Lindi na nchi kwa ujumla katika kupambana na changamoto mbalimbali zikiwemo za upungufu wa walimu, madaktari, wauguzi na watumishi wengi kwa kuwa baada ya kumaliza masomo yao watajiunga na vyuo kusomea taaluma mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad