HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, May 5, 2019

Wananchi wanapaswa kujua Historia yao- Balozi Seif

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Wananchi wanapaswa kujua Historia yao katika dhana nzima ya kuendelea kulinda Uhuru wao, Heshima, Utamaduni na hata mazingira yao yanayowazunguuka ya kila siku.

Alisema Binaadamu asiyejua Historia yake kamwe anakuwa Mtumwa wakati wote akiendelea kutawaliwa kifikra jambo ambalo ni hatari katika maisha yake yanayomuhusu.

Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo alipofanya ziara fupi ya kuyakagua Mahandaki Mawili ya Mangapwani yaliyokuwa yakitumika kuhifadhia Watumwa ambayo kwa sasa yamekuwa sehemu muhimu ya kujifunza Historia ya Biashara hiyo iliyopigwa marufuku tokea Karne ya 18.

Alisema Zanzibar ilikuwa kituo muhimu cha Historia iliyounganisha sehemu nyingi Duniani historia ambayo Taasisi inayosimamia masuala hayo ambayo ni Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale ina jukumu la kusimamia vyema maeneo yote muhimu ili Wageni pamoja na Wananchi wapate fursa ya kujifunza zaidi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar pia aliwakumbusha Vijana wanaosimamia maeneo hayo kufanya jitihada ya kujifunza Historia kamili ili kuepuka tabia ya kutoa Taarifa zisizo na uhakika wa Historia ya maeneo wanayofanyia kazi.

Akitoa ufafanuzi Msimamizi wa Mahandaki ya Mangapwani Makame Omar Said alisema maumbile ya eneo hilo muda wote yamekuwa ya kujificha kutokana na hali halisi ya biashara yenyewe ya Utumwa ilivyokuwa ikifanywa kwa kujificha.

Makame alisema utafiti unaonyesha wazi kwamba bado idadi ya Wazawa kufika eneo hilo kwa ajili ya kujifunza Historia yake ni ndogo ikilinganishwa na Wageni pamoja na Wasomi wa fani za Kihistoria.

Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale anayesimamia Utalii na Mambo ya Kale Dr. Amina Ameir Issa alimueleza Balozi Seif kwamba Idara ya Mambo ya Kale ilianzishwa Mnamo Mwaka1920.

Dr. Amina alisema hatua hiyo ilifuatiwa na kutungwa kwa Sheria ya Mambo ya Kale Mnamo Mwaka 1941 ikiwa chini ya uangalizi wa Idara ya Mambo ya Kale ikiwa na lengo la kusimamia maeneo Saba ya Kihistoria hapa Zanzibar.

Aliyataja baadhi ya Maeneo hayo kuwa ni pamoja na Mahandaki ya Mangapwani,Msikiti Mkongwe wa Kizimkazi, Mji wa Makutani uliopo katika Kisiwa cha Tumbatu pamoja na Mji wa Mwinyimkuu uliopo Dunga.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale anayesimamia Utalii na Mambo ya Kale alifahamisha kwamba Mahandaki ya Mangapwani yana bahati kubwa ya kutembelewa na Wageni wengi, Watalii, Wanafunzo pamoja na Watafiti ikilinganishwa na sehemu nyengine za Kihistoria zilizopo Zanzibar.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale Bibi Khadija Bakari Juma alisema Wizara hiyo kwa sasa tayari imeshaandaa mpango maalum wa kushajiisha Utalii wa ndani ili kuimarisha zaidi mapato ya Taifa.

Bibi Khadija alisema mpango huo umeaanza kufanya kazi kwa kuwahusisha watendaji wa Wizara hiyo kama muelekeo wa ushajiishaji ili kuungwa mkono ya Wizara nyengine na baadae Wananchi hapa Nchini.

Katibu Mkuu Habari ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa uamuzi wake wa kutenga Bajeti Maalum kila Mwaka inayolenga kuhudumia Uhifadhi wa Maeneo ya Kihistoria hapa Nchini jambo ambalo limeleta matokeo mazuri katika usimamizi wa maeneo hayo muhimu.

Akielezea changamoto zinayoyakabili maeneo mengi ya Kihistoria Nchini Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini “B” Nd. Rajab Ali Rajab alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba uhaba wa wafanyakazi ni tatizo kubwa linalofaa kuangaliwa na Serikali pamoja na Taasisi inayosimamia maeneo hayo.

Nd. Rajab alisema ufinyu huo wakati mwengine hutoa mwanya kwa wahalifu kufanya hujuma katika maeneo hayo ambayo kwa namna yoyote ile yanapaswa kuheshimiwa na kuenziwa kwa vizazi vya sasa na vile vijavyo.

“ Yapo matendo mabaya wakati mwengine hufanyika ya uharibifu a maeneo ya Hifadhi kama uchafuzi wa mazingira kutokana na kukosa usimamizi imara wa Watendaji”. Alisisitiza Mkuu huyo wa Wilaya ya Kaskazini “B”.

Zanzibar iliyokuwa Kituo cha Biashara ya Utumwa katika Mwambao wa Afrika Mashariki ilisimamisha Biashara hiyo chini ya Utawala wa Uingereza Mnamo Mwaka 1873 licha ya baadhi ya Wafanyabiashara kuendelea kufanya biashara hiyo kwa siri. 
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akifanya ziara ya kukagua Mahandaki Mawili ya Mangapwani yaliyokuwa yakitumika kuhifadhia Watumwa ambayo kwa sasa yamekuwa sehemu muhimu ya kujifunza Historia ya Biashara hiyo iliyopigwa marufuku tokea Karne ya 18.
 Balozi Seif Ali Iddi akipewa maelezo ya Biashara ya Utumwa ilivyokuwa ikufanyika katika Mahandaki ya Mangapwani Mkoa wa Kaskazini Unguja.
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale anayesimamia Utalii na Mambo ya Kale Dr. Amina Ameir Issa akielezea jitihada zinazochukuliwa na Wizara kuyasimaia vyema Mahandaki ya Mangapwani.
 Balozi Seif akiuagiza uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale pamoja na ule wa Wilaya kuendelea kuyahifadhi Mahandaki ya Mangapwani ili yaendelee kutoa huduma za Kihistoria. Picha na – OMPR – ZNZ.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad