HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 31, 2018

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kuongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika na China (FOCAC) mjini Beijing

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika na China (FOCAC) utafanyika Beijing kuanzia tarehe 01 hadi 04 Septemba, 2018.

Ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo utaongozwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa. Viongozi wengine watakaoshiriki Mkutano huo ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga; Mhe. Khalid Salum Mohamed, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mhe. Rashid Ali Juma, Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, na Viongozi wengine Waandamizi.

Mkutano huo utafunguliwa na Rais wa China, Mhe. Xi Jinping ambaye pia ni Mwenyekiti wa jukwaa hilo, kwa kushirikiana na Mwenyekiti Mwenza, Rais wa Afrika Kusini, Mhe. Matamela Cyril Ramaphosa, utahudhuriwa pia na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika ambaye pia ni Rais wa Rwanda, Mhe. Paul Kagame, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. Antonio Guterres na Mwenyekiti wa Kamisheni ya Afrika ambaye pia ni Rais wa Chad, Mhe. Moussa Faki Mahamat. Mkutano huo pia utashuhudia uchaguzi wa Mwenyekiti Mwenza mpya kutoka Afrika.

Kaulimbiu ya Mkutano wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika kwa mwaka 2018 ni “China na Afrika: Kuelekea Jumuiya Imara kwa mustakabali wa wote kupitia ushirikiano kwa manufaa ya wote” (China and Africa: Toward an Even Stronger Community with a Shared Future through Win-Win Co-operation).

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali utatanguliwa na kikao cha Makatibu Wakuu kitakachofanyika tarehe 01 Septemba, 2018. Kikao hicho pamoja na mambo mengine kitapitia agenda za mkutano huo na kuziwasilisha kwenye kikao cha Mawaziri kitakachofanyika tarehe 02 Septemba, 2018.

Mkutano wa Jukwaa la Ushirikiano kati Afrika na China pamoja na mambo mengine utajadili namna ya kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na China na kufanya mapitio ya mikakati ya pamoja ya maendeleo iliyopo kati ya Afrika na China. Jukwaa hilo ambalo lilianzishwa mwaka 2000 huwaleta pamoja viongozi wa Afrika na China kujadili masuala ya ushirikiano na maendeleo na kutathmini utekelezaji wa makubaliano mbalimbali yanayofikiwa kati yao.

Aidha, masuala ya ushirikiano katika uendelezaji Miundombinu kama Barabara, Reli, Bandari na upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa Bara la Afrika yatajadiliwa kwa kina. Agenda nyingine itahusu kilimo cha kisasa ambapo China itatoa uzoefu wake katika kutumia sayansi na ubunifu wa kiteknolojia katika kufikia uzalishaji wenye tija na kuongeza thamani kwa mazao ili kuwa na soko la uhakika.

FOCAC 2018 pia itajadili masuala ya biashara na uwekezaji ambapo kwa kuona umuhimu huo, Mhe. Xi Jinping, Rais wa China atafungua rasmi Mkutano wa Jukwaa la Biashara kati ya China na Afrika utakaofanyika tarehe 03 Septemba, 2018.

Mkutano wa kwanza wa Wakuu wa Nchi wa Jukwaa hili ulifanyika Beijing mwaka 2006 na Mkutano wa Pili ulifanyika nchini nchini Afrika Kusini mwaka 2015.

Wakati wa Mkutano wa pili, China ilitangaza mpango kabambe wa kuhamasisha mapinduzi ya viwanda na kilimo cha kisasa kwa Afrika wenye gharama ya Dola za Marekani bilioni 60 katika utekelezaji wake. Kufuatia ushirikiano kupitia Jukwaa hilo biashara kati ya China na Afrika imeongezeka pamoja na ongezeko la ushirikiano wa kiutamaduni na biashara baina ya watu wa China na Afrika.

Pembezoni mwa Mkutano huo, Tanzania na China zimeandaa Kongamano la Biashara ambalo litafunguliwa rasmi na Mhe. Waziri Mkuu tarehe 02 Septemba, 2018. Kongamano hilo ambalo litajadili kwa kina masuala ya uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na China litashirikisha takribani makampuni 80 kutoka nchi hizi mbili.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dodoma.



30 Agosti 2018

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad