Monday, January 9, 2017

USIRI WATAWALA YANGA NA SIMBA, KUVAANA KESHO


Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
IKIWA imebakia  siku moja kufikia mtanange wa watani wa jadi kuelekea nusu fainali ya kombe Mapinduzi, viongozi wa timu hizo mbili zimegoma kuzungumza na vyombo vya habari na zaidi wakisema mpira ni dakika 90.

Simba wakiingia msituni wakitoka pale walipokuwa wanakaa toka kuanza kwa mashindano haya Yanga wameendelea kusalia pale pale huku wakiwaficha wachezaji wao na kuamua kufanya mazoezi usiku kwenye Uwanja wa Amani.

Mashabiki wa pande zote mbili wamejinadi kuweza kuondoka na ushindi katika mchezo huo huku kwa upande wa Simba wakijiamini zaidi wakiwa na imani na kikosi chao kwa kuweza kupata matokeo mazuri zaidi, Yanga wakiwa na uchungu wa kupoteza katika mchezo wao wa hatua ya makundi dhidi ya Azam.

Mechi hiyo ya nusu fainali ya watani wa jadi itapigwa kesho majira ya saa 2:15 katika uwanja wa amani na kabla ya mchezo huo kutakuwa na nusu fainali ya kwanza kati ya Azam na Taifa Jang'ombe. 


Jang’ombe inakutana na Azam FC katika mchezo huo utakofanyika kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar kesho Jumanne saa 10.15 jioni, baada ya kumvua taji bingwa mtetezi wa michuano hiyo, URA ya Uganda kwa kuifunga bao 1-0 katika mchezo wake wa mwisho wa Kundi A.

Mara ya mwisho Azam FC kukipiga na Jang’ombe ilikuwa ni Julai 31 mwaka jana kwenye mchezo wa kirafiki wa maandalizi ya msimu huu, ambapo mabingwa hao wa Ngao ya Jamii walishinda bao 1-0 lililowekwa kimiani kiufundi na mshambuliaji aliyekuwa katika majaribio Mburundi Fuadi Ndayisenga.


No comments:

Post a Comment