HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, May 19, 2018

WATENDAJI WAKUU NA WAJUMBE WA BODI WAPIGWA MSASA NA OFISI YA MSAJILI HAZINA

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Amina Shabani akizungumza na watendaji wakuu na wajumbe wa bodi katika mafunzo ya siku moja kuhusu uwajibikaji na utendaji katika taasisi na mashirika ya Umma yaliyoendeshwa na ofisi ya Msajili wa Hazina.

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
WATENDAJI wakuu na wajumbe wa bodi za taasisi na mashirika ya umma wamepatiwa mafunzo ya siku moja kuhusu uwajibikaji na utendaji katika taasisi na mashirika wanayofanyia kazi yaliyoendeshwa Ofisi ya Msajili wa Hazina nchini.

Mgeni rasmi wa mafunzo hayo Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Amina Shaban amesema kuwa Katika kutekeleza lengo hili, walivunja SCOPO mwaka 1992 na kuhamishia majukumu yake mengi Ofisi ya Msajili wa Hazina na wakatunga Sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1992 na marekebisho yake ya mwaka 1993 na 2010 ili kuboresha usimamizi na kuleta tija katika Taasisi na mashirika yake.

Amina ammesema kuwa Mwezi Mei 2010, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilirekebisha Sheria ya Msajili wa Hazina Sura 370 ya mwaka 2002 na kuifanya Ofisi inayojitegemea ili kuboresha uendeshaji na usimamizi wa Taasisi na Mashirika ya Umma katika dhana nzima ya kuruhusu ushindani katika soko la Uchumi huria.

"Tumelazimika leo kuwa na mafunzo haya ili kukumbushana Majukumu ya

Watendaji wa Mashirika na Taasisi za Umma Pamoja na Bodi za Wakurugenzi kama mnavyofahamu, kufuatana na Sheria mbalimbali zinazounda Mashirika ya Umma, kila Shirika lina Mtendaji Mkuu pamoja na Bodi ya Wakurugenzi ambayo ina wajibu wa kuiongoza Menejimenti katika utekelezaji wa majukumu ya Shirika husika,"amesema Amina.

"Kufanikiwa kwa Mashirika ya Umma kunategemea sana uimara wa Bodi za Wakurugenzi ambazo zinazingatia majukumu na mipaka yake ya kazi. Bodi ya wakurugenzi inawajibika kufuatilia, kusaidia na kuiwezesha Menejimenti ya Mashirika/Taasisi za Umma kuinua tija na kuongeza ufanisi,"

Amesema kuna changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika baadhi ya Mashirika/Taasisi za Umma, ni Bodi kujiingiza katika mambo ya kiutendaji ya kila siku ya Shirika. Aidha, baadhi ya Wenyeviti wa Bodi wanafanya vitendo vinavyoashiria kwamba wao ni

Wenyeviti Watendaji badala ya kuwa Wenyeviti wa Bodi.

Tatizo hilo limejidhihirusha kuwa baadhi ya Wenyeviti wanadai nyenzo na marupurupu ambayo si stahili yao, kwa mfano Ofisi, nyumba, usafiri na posho mbalimbali, bodi kufanya maamuzi, kama vile kuidhinisha mikataba bila Msajili wa Hazina na Wizara Mama kutoa idhini, kuamuru uhamisho wa watumishi na kuitisha vikao vya watumishi huku Menejimenti kutokujulishwa na kurekebisha au kuidhinisha matumizi ya fedha za Shirika bila kufuata kanuni.

Mbali na hilo pia wanafanya miongozo ya usimamizi wa fedha za umma, pamoja na ununuzi.

Mashirika na Taasisi zote za Serikali zimetakiwa zihakikishe zinazingatia sheria, kanuni na taratibu zote zilizopo ikiwa ni pamoja na maagizo yanayotolewa na Serikali mara kwa mara sambamba na Sheria ya Msajili wa Hazina (Treasury Registrar ) (Powers and Functions) Sura 370 ya Mwaka 2002 na kama ilivyorekebishwa 2010,sheria ya Mashirika ya Umma (The Public Corporations Act) ya mwaka 1992 na marekebisho yake na Nyaraka mbalimbali zinazotolewa na Ofisi ya Msajili wa Hazina na Serikali kwa ujumla.

Pili Kuhakikisha kuwa Shirika linafuata matakwa yote ya Sheria na kuendesha Shirika kwa ufanisi. Hii ni pamoja na kuhakikisha kuwa Hesabu za Shirika zinakaguliwa kwa mujibu wa sheria,mapendekezo ya maoni ya wakaguzi wa hesabu kushughulikiwa na hoja za wakaguzi hao kujibiwa kikamilifu.

Kwa upande wa Uwajibikaji , Kila Bodi ina wajibu wa kutoa taarifa kwa mwenye mali kuhusu maamuzi makubwa yaliyochukuliwa au yanayotarajiwa kuchukuliwa na Bodi husika hususan, maamuzi yenye mwelekeo wa kisera au yenye maslahi ya kitaifa.

Kaimu Msajili wa Hazina Dkt Maftah Bunini amesema kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/18, Ofisi ya Msajili wa Hazina imeendelea kutekeleza jukumu lake la usimamizi wa Bodi kwa kuhakikisha zinakuwa hai na kuwa na Wajumbe wenye weledi wa kutosha. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2017, Taasisi na Mashirika ya Umma yapatayo 181 (77%) kati ya 234 yalikuwa na Bodi zilizo hai.

Aidha, Taasisi na Mashirika ya Umma yapatayo 53 hayakuwa na Bodi za Wakurugenzi. Ofisi ya Msajili wa Hazina imeandaa nyenzo ya Tathmini ya utendaji kazi wa Bodi (Board Evaluation Tool). Nyenzo hii inatumiwa na Wajumbe wa Bodi kutathmini utendaji wa kila mmoja wao na kufanya tathmini ya Bodi nzima kwa ujumla katika kipindi cha mwaka husika na kipindi chote wanachohudumu katika Bodi hiyo.

Mafunzo hayo yaliweza kuleta tija kwa wajumbe wa bodi na watendaji wakuu kutoka katika taasisi na mashirika ya Umma kuweza kufahamu majukumu yao na wajibu.
Kaimu Msajili wa Hazina Dkt Maftah Bunini akizungumza wakati wa mafunzo ya uwajibikaji kwa watendaji wakuu na wajumbe wabodi yaliyoendeshwa na ofisi ya Msajili wa Hazina.
 Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Taifa (BMT) Leodegar Tenga akichangia jambo wakati wa mafunzo ya uwajibikaji kwa watendaji wakuu na wajumbe wa bodi.
Watendaji wakuu na wajumbe wa bodi wakifuatilia mafunzo hayo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad