HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 16, 2021

RC RUVUMA ATOA MAAGIZO MAZITO

 
Na Yeremias, Ngera Ngera, Namtumbo

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Brigedia Generali Wilbert Ibuge ametoa maagizo mazito kwa viongozi wa wilaya ya Namtumbo kwa kuwataka ifikapo septemba, 30 mwaka huu 2021 wawe wamekamilisha kutekeleza maagizo ya kamati ya kudumu ya bunge pamoja na kuhakikisha hoja ambazo hazijafungwa zinafungwa.

Akizungumza kwenye kikao maalumu cha baraza la madiwani cha kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali juu ya hoja na mapendekezo ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa hesabu za mamlaka za serikali za mitaa kwa mwaka wa fedha 2019/2021 katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Ibuge amesema ifikapo tarehe 30 septemba mwaka huu katibu tawala wa mkoa bwana Stephen Mashauri Ndaki awasilishe taarifa ofisini kwake namna alivyosimamia Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo kutekeleza maagizo ya kamati ya kudumu ya bunge pamoja na kufunga hoja ambazo hazijafungwa.

Ibuge alidai kuwepo kwa hoja 78 ambazo hazijafungwa na maagizo sita ya LAAC kunaonesha dalili kuwa menejimenti ya halmashauri haizipi uzito unaostahili katika kujibu hoja na hivyo kukosa majibu yanayojitosheleza ili hoja iweze kufungwa baada ya kufanyiwa uhakiki alisema Ibuge.

Kwa mujibu wa taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo imepata hati yenye mashaka na msingi wa kupata hati yenye mashaka ni kutokana na sababu ya hati za madai zilizoidhinishwa kwenye mfumo wa ukusanyaji mapato (LGRCIS) bila ya kuwa na nyaraka toshelezi ya shilingi 191,935,660.

Diwani wa kata ya Mkongo bwana Daniel Nyambo pamoja na mambo mengine katika kikao hicho alisema madiwani wanaridhia kuwa maoni ya kamati ya fedha ndio yatumike kuwa maoni ya baraza maalumu la kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali katika utekelezaji wa mapendekezo ya hoja za ukaguzi kwa mwaka 2019/2020 katika halmashauri ya wilaya ya Namtumbo.

Naye Deogratius Waijah mkaguzi mkuu wan je mkoa wa Ruvuma alisisitiza kuwa Halmashauri ijipange kwa ukaguzi ujao kwa kuwa mwisho wa ukaguzi ni mwanzo wa ukaguzi mwingine hivyo ni vyema kujiweka tayari kwa ukaguzi na kuonesha ushirikianao kwa timu ya wakaguzi itakayofanya kazi Namtumbo alisema Waijah.

Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo kwa miaka minne mfululizo 2015/2016,2016/2017,2017/2018 na 2018/2019 ilipata hati safi na mwaka 2019/2020 Halmashauri yawilaya Namtumbo imepata hati yenye mashaka.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad