Thursday, October 17, 2019

WANAUME WAASWA KUWASAIDIA WANAWAKE KATIKA UZALISHAJI NA UTUNZAJI WA CHAKULA

 Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Bi. Coletha Shayo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Gehandu kuhusu umuhimu wa wanaume kushirikiana na wanawake katika kuzalisha chakula wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.
 Katibu Tawala Wilaya ya Hanang Bw Paulo Bura akizungumza na wananchi wa kijiji cha Gehandu na kusisitiza wanaume kutouza chakula na kuicha familia ikiwa na njaa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.
 Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, na Watoto Bw. Abel Palapala akitoa elimu kwa wanakijiji wa Gehandu kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi kwa wananchi wanaoishi vijijini wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.
 Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, na Watoto Bi. Silvia Siriwa akieleza uhusisano ulipo kati ya uzalishaji na mwanamke kwa wananchi wanaoishi vijijini wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara. Pix 5 Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Gehandu wakifuatilia hotuba mbalimbali wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara. Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WAMJW


Wanaume nchini Tanzania wameaswa kuwasaidia wanawake katika shughuli za maendeleo hasa katika uzalishaji wa chakula katika kaya ili kuondokana na upungufu wa chakula katika familia.

Hayo yamesemwa na Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Bi. Coletha Shayo katika Kijiji cha Gehandu kilichopo katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani ikiwa na kauli mbiu isemayo " Lishe Bora kwa Ulimwengu usio na njaa"

Bi. Coletha ameongeza kuwa wanaume ni nguzo muhimu kwa familia na kuwataka wanaume kutelekeza familia zao wakati wa uhaba wa chakula bali kujipanga pamoja kwa kuweka chakula cha akiba.

Amewataka wanawake na Wanaume wa Kijiji cha Gehandu kuchangamkia fursa zilizopo ikiwemo uwepo wa ardhi nzuri na wataalam wa kilimo na mifugo ili kulima kilimo cha bora na kuwa na ufugaji wa kisasa.

Aidha amewataka wananchi hao kushirikiana katika kuhakikisha wanakuwa na mafanikio katika shughuli za kilimo na ufugaji ili kusaidia kuleta maendeleo katika kijiji chao.

"Niwatake wananchi wa kijiji hiki kuzingatia utunzaji wa chakula hasa suala la lise bora katika familia ili kuondokana na tatizo la udumavu kwa Watoto" alisisitiza Bi. Coletha

Naye Katibu Tawala Wilaya ya Hanang Bw Paulo Bura amesisitiza wanaume kushirikiana na wanawake kuzalisha chakula kwa ajili ya chakula na kuuza ili kujenga uchumi wa kaya na taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa wanaume walio wengi wamekuwa wakiona fahari kuwa na mifugo mingi huku familia zao zikiwa katika hali duni hivyo amewataka kuitumia mifugo kuwasaidia kupata chakula, kununua mashamba na kusomesha watoto.

"Kuna mila za kuwa na mifugo mingi katika jamii nyingi za wafugaji huku wakikosa huduma nyingine kama chakula elimu na afya tusiifanye mifugo fahari itusaidie katika kuendeleza familia zetu" alisema Bw. Bura

Akielezea mikakati ya Wizara yenye dhamana kwa wanawake Mratibu wa Maadhimisho kutoka Wizara husika Bi. Silyvia Siriwa amesema Wizara imejikita katika utoaji wa elimu kwa wanawake itakayowasaidia kujikwamua kiuchumi na pia kuondokana na vitendo vya ukatili katika jamii.

"Mwanamke akiwezeshwa kiuchumi katika jamii anaondokana na vitendo ukatili wa kijinsia na kuisaidia jamii inayowazunguka" alisisitiza Bi. Silyvia

Naye Mkazi wa Kijiji cha Gehandu Bi. Pili Mussa amesema kuwa wanaume wamekuwa wakiuza mazao bila kuwashirikisha na kusababisha njaa katika familia nyingi na hata kuzikimbia familia zao wakati wa uhaba wa chakula kwa kigezo cha kwenda kutafuta maisha.

Kwa upande Mkazi wa Kijiji cha Gehandu Bw. Samwel Arajiga amesema kuwa baadhi ya wanaume wamekuwasababu ya kuleta njaa katika familia kwa kuuza mazao yote na kutumia pesa kunywe pombe hivyo ameomba elimu zaidi kutolewa kuhusu umuhimu wa kutunza chakula katika familia.

Amesisitiza utolewaji wa elimu ya kilimo bora na lishe bora kwa wananchi wa vijijini ili kuondokana na tatizo la udamavu kwa kuzingatia ulaji bora kwa watoto na familia zao.

No comments:

Post a Comment