HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 9, 2019

MBUNGE JUMAA ATOA KONTENA LA VIFAA TIBA MLANDIZI

NA MWAMVUA MWINYI, KIBAHA VIJIJINI 
MBUNGE wa jimbo la Kibaha Vijijini, mkoani Pwani, Hamoud Jumaa ametoa kontena la futi 40, lenye vifaa tiba mbalimbali pamoja na baadhi ya samani za shule ambalo limegharimu kiasi cha sh. milioni 400.

Akikabidhi kontena hilo la vifaa kwa mganga mkuu wa wilaya ya Kibaha Ibrahim Isaack, mbunge Jumaa alisema, msaada huo unalenga kukabiliana na changamoto ya upungufu wa vifaa tiba uliopo katika kituo cha afya cha Mlandizi.

"Kutokana na jitihada za serikali na Rais Dkt. John Magufuli ambazo anazichukua kutatua matatizo yaliyopo katika sekta ya afya, ambapo zimeshatolewa sh. milioni 400 za kukarabati ,kupanua ama kujenga majengo ya vituo vya afya, "

"Nami nimeona niunge juhudi za Rais Dkt. Magufuli kukabiliana na changamoto hizo ili kuboresha huduma zinazotolewa kwenye kituo cha afya na zahanati "alisema Jumaa. 

Aidha Jumaa, alisema kipindi cha nyuma alitoa kontena la vitabu mbalimbali ambavyo vilisambazwa katika shule za msingi na sekondari, lakini kwa sasa ameleta samani zitakazotumika kwenye baadhi ya shule hizo.  Aliwahakikishia wananchi wa jimbo hilo, anaendelea kusimamia kero na ahadi alizowahi kuzitoa .

Akipokea msaada huo, mganga mkuu wa wilaya ya Kibaha, Dokta Ibrahim Isaack,alimshukuru na kudai msaada alioutoa umekuja wakati muafaka kwani wakati serikali ikiboresha miundombinu,mbunge huyo  amesaidia vifaa tiba. 

Dokta Isaack, alisema mbali ya kuletwa kwa kontena hilo, pia Jumaa alichangia na kusimamia ujenzi wa uzio kwenye kituo cha afya Mlandizi, kero ambayo ilikuwa ikiwakera wagonjwa wengi. 

Hata hivyo, alitaja baadhi ya changamoto ambazo bado zinawakabili ni upungufu wa watumishi, vituo vya afya, zahanati kuwa  umbali mrefu na huduma za dharura kupatikana umbali kwani zipo nyingine ambazo zipo umbali wa kilometa 100 ambapo husababisha usumbufu kwa wagonjwa hasa wajawazito ama wanaokwenda kujifungua.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad