HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, December 10, 2018

LUGOLA AWAOMBA WANANCHI KUCHANGIA UJENZI VITUO VYA POLISI KUIMARISHA USALAMA NCHINI

Na Felix Mwagara, (MOHA) MARA.

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka Watanzania wawe na utamaduni wa kuchangia ujenzi wa vituo vya polisi kama wanavyochanga katika michango mingine ya maendeleo nchini.

Lugola amesema ni mara chache sana kuona wananchi wanachangia ujenzi wa kituo cha polisi katika maeneo wanayoishi kutokana na baadhi ya Watanzania wanaamini vituo vya polisi ujengwa na serikali pekee jambo ambalo halina msingi la linakwamisha maendeleo ya nchi.

Akizungumza na mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Kibara B, Mwibara, Wilaya ya Bunda, Mkoani Mara, Lugola amesema ili usalama uzidi kuimarishwa katika maeneo mbalimbali nchini, wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika ujenzi wa vituo vya polisi.

Lugola alisema katika mikutano yake ya nchi nzima anayoendelea kuifanya, atazidi kuwahamasisha wananchi waweke utamaduni wa kuchangia kwa ajili wa ujenzi wa vituo hivyo ili ulinzi upatikane sehemu mbalimbali nchini na kupunguza au kuyaondoa kabisa matukio ya uhalifiu.

“Nimeona wananchi wakichanga ujenzi wa zahanati, shule pamoja na michango mingine ya maendeleo, lakini wanakua wazito kabisa katika kuchangia ujenzi wa kituo cha polisi katika eneolao wanaloishi,” alisema Lugola.

 Lugola aliwataka wananchi kuungana na Serikali ya Rais Dk John Pombe Magufuli ambayo inalenga kuleta maendeleo katika kuibadili nchi, hivyo ushirikiano na wananchi unahitajika ili nchi iwezwe kusonga mbele zaidi.

“Tunatarajia kujenga kituo cha Polisi cha kisasa cha ghorofa katika eneo hili la Kibara, lakini wananchi mnapaswa kutoa michango yenu ili kufanikisha hili, tuweke utamaduni wa kuchanga jamani, si hapa tu Kibara jimbo la Mwibara bali wananchi wote nchini jengeni utamaduni wa kutoa michango ujenzi wa vituo vyenu vya polisi pamoja na nyumba za makazi ya hawa walinda usalama wenu,” alisema Lugola.

Aidha, Lugola aliwataka wananchi hao waongeze kasi katika maandalizi ya kilimo kwasababu mvua tayari zimeanza kunyesha, hivyo waongeze nguvu za kulima mazao ya chakula na biashara ili kuithibiti njaa isitokee katika eneo hilo.  

Lugola anaendelea na ziara yake kwa kutembelea vijiji vyote zilizopo katika kata 14 zilizopo jimboni kwake akisikiliza kero za wananchi pamoja na kuhamasisha kilimo cha mazao ya pamba, mahindi, mpunga, viazi na mengineyo ambayo wakazi wa jimbo lake wanalima mazao hayo kwa wingi.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Kibara B, Mwibara, Wilaya ya Bunda, Mkoani Mara, leo.  Lugola aliwaomba wananchi wa kijiji hicho wachangie ujenzi wa kituo vya polisi katika eneo hilo ili kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kulia), akimsikiliza Mkazi wa Kijiji cha Sikiro, Kata ya Iramba, Mwibara Wilayani Bunda, Mkoa wa Mara, Elia Majinge alipokua anatoa kero yake katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji hicho, jimboni humo, leo. 
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kibara B, Mwibara, Wilaya ya Bunda, Mkoani Mara, leo.  Lugola aliwaomba wananchi kijijini hapo wachangie ujenzi wa kituo vya polisi ili kuimarisha ulinzi zaidi nchini. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad