HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, December 4, 2018

DKT. MABODI AWATAKA WATENDAJI WA SERIKALI ZA MITAA KUWA KARIBU NA WANANCHI

Na Is-Haka Omar, Zanzibar
WATENDAJI wa Serikali za Mitaa nchini wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya ziara za kiutendaji kwa wananchi wa ngazi zote ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto zinazowakabili wananchi. Rai hiyo ameitoa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi katika mwendelezo wa ziara zake za kukagua utekelezaji wa Ilani katika Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja.

Amesema lazima watendaji na viongozi waliopewa dhamana ya kusimamia mfumo wa ugatuzi washuke kwa wananchi kwa lengo la kufuatilia masuala mbali mbali yatakayosaidia kumaliza changamoto zinazowakabili wananchi katika ngazi za serikali za mitaa. "Lengo la Serikali Kuu kushusha madaraka katika Serikali za Mitaa kupitia dhana ya ugatuzi ni kuongeza ufasini wa uimarishaji wa huduma za kijamii kwa wananchi, hivyo watendaji nyote mlioaminiwa na kupewa dhamana ya kuwahudumia wananchi lazima muwe katibu na jamii", amesisitiza Dk.Mabodi.

Katika maelezo yake Naibu Katibu Mkuu huyo, amewataka wamewasihi watendaji hao kuwa wabunifu katika kuibua miradi mbali mbali ya kijamii inayoweza kuongeza ufanisi wa kutoa huduma bora kwa wananchi. Pia Dk. Mabodi kupitia ziara yake hiyo ameelezea kuridhishwa kwake na utendaji mzuri wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' katika kutekeleza vizuri miradi inayotekelezwa kupitia ugatuzi.

Dk. Mabodi aliwasihi wananchi kuendelea kuthamini na kuamini juhudi kubwa za kimaendeleo zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Saba ya Zanzibar inayoongozwa na Dk. Ali Mohamed Shein, kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020. Naibu Katibu Mkuu huyo akiwa katika Kijiji cha Zingani kinachokabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji safi na Salama, na kuahidi kuwapatia masine  ya maji ili kusaidia upatikanaji huduma hiyo.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' Mussa Ali Makame, amesema katika ukusanyaji wa mapato katika mwaka 2018/2019 wamekisia kukusanya shilingi milioni 869,300,000 hadi Novemba wamekusanya kiasi cha shilingi milioni 157,697,081 sawa na asilimia 18. Amesema Halmashauri hiyo imetoa mafunzo kwa wakulima 144 ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula cha biashara.

Aidha ameeleza kuwa wametoa mafunzo kwa wafugaji 1,027 wa ng'ombe na mbuzi kwa lengo la kuwajengea uelewa wa matumizi ya huduma ya chanjo. Mussa amesema jumla ya Shule 32 za Wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja ambapo wanafunzi 6,158 wa maandalizi wamepatiwa huduma ya lishe kwa mwaka wa fedha kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018 pamoja na 2018/2019.

Akizungumza Mjumbe wa Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar Amini Salmin Amour, amewataka wataalamu wa fani mbali mbali waliopelekwa katika mfumo wa ugatuzi kutumia ujuzi wao kuwaelimisha wananchi juu ya masuala ya kilimo bora, ufugaji, uvuvi sambamba na kuhakikisha miradi yote inayotekelezwa inawanufaisha watu husika.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Idd Ali Ame, amempongeza Naibu Katibu Mkuu huyo Dk.Mabodi kwa ziara yake hiyo ambayo ameitaja kuwa imeongeza ari na kasi ya watendaji kutatua kero za wananchi kwa wakati. Kwa upande wake Mkaazi wa Kijiji cha Mbuyu Tende Ramadhan Ali Mcha ameeleza kuwa mfumo wa ugatuzi umewasaidia wananchi kupata huduma muhimu za kijamii.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Zanzibar alitembelea maeneo mbali mbali yaliyotekelezwa miradi kupitia mfumo wa ugatuzi yakiwemo kukagua ujenzi wa madarasa matano katika shule ya Sekondari Gamba, mradi wa umeme shehia ya Mbuyu tende, nasari ya kivunge, kituo cha misitu Kivunge, kutembelea pamoja na mradi wa huduma za maji na choo cha jamii katika kijiji cha Bwekunduni.

Maeneo mengine yaliyokaguliwa miradi hiyo ni ujenzi wa Nyumba ya Madaktari Shehia ya shehiya ya Tazari, mradi wa kukusanya taka taka na ujenzi wa madarasa ya maandalizi Nungwi pamoja na kukagua kikundi cha ushirika chenye mashine ya kisasa ya kukoboa mpunga huko Kisongoni.
 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi akizungumza na Watendaji wa Halmashauri ya Wilaya Kaskazini 'A' katika mwendelezo wa ziara yake katika Mabaraza ya Manispaa na Halmashauri za Wilaya Unguja.
 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi akionyesha moja ya ripoti za ukaguzi wa miradi ya mfuko wa maendeleo wa majimbo huku akisisitiza uwajibikaji na uwazi juu ya matumizi ya fedha zinazotolewa na Wabunge na Wawakilishi Zanzibar.
 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi akiwa na wananchi wa shehia ya Mbuyu Tende wakielekea kukagua mradi wa umeme na maji katika kijiji cha Zingani.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi akigagua mashine ya kukoboa mpunga aina ya G-20 inayomilikiwa na kikundi cha ushirika wa 'Nguvu kazi tusizembee' huko Shehia ya Kisongoni Wadi ya Kinyasini Unguja.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad