HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 6, 2018

SIMIYU YAZINDUA MFUMO WA MSHITIRI MMOJA KATIKA DAWA NA VIFAA TIBA , JAZIA

Na Stella Kalinga, Simiyu
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini  amezindua rasmi mfumo wa ununuzi wa dawa na vifaa tiba kupitia kwa mshitiri mmoja wa mkoa ujulikanao kama JAZIA, uliobuniwa kuboresha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, vifaa vya maabara na uchunguzi katika vituo vya kutolea huduma za afya vya Serikali ngazi ya Mkoa na Halmashauri.

Akizindua mfumo huo Novemba 05, 2018  Sagini amesema mfumo wa JAZIA si mbadala wa Bohari ya Dawa (MSD) bali unalenga kuziba upungufu wa dawa, vifaa tiba, vifaa vya maabara na uchunguzi katika Bohari ya Dawa (MSD).

“JAZIA ni mfumo uliobuniwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na wataalam washauri ili kuweza kuboresha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, vifaa vya maabara na uchunguzi katika vituo vya kutolea huduma za afya vya Serikali ngazi ya Mkoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa, JAZIA si mbadala wa MSD bali ni msaidizi wa MSD inapokuwa haina bidhaa husika.” alisema.

Aidha, Sagini alibainisha kuwa mfumo huu utasaidia kupunguza gharama na bei ya upatikanaji wa dawa kwani bei za dawa na vifaa tiba zitalingana na bei ya soko na sio matakwa binafsi ya wazabuni.

Aliongeza kuwa mfumo huo utapunguza urasimu uliokuwepo wa namna ya kununua dawa nje ya MSD na hivyo kusaidia dawa kupatikana kwa muda mfupi huku akiwataka Waganga wafawidhi wa vituo vyote vya kutolea huduma za afya kuagiza dawa na vifaa tiba mapema wanapoona vinapungua kabla ya kusubiri vifaa hivyo na dawa kuisha kabisa.

Kwa upande wake Mratibu wa Mfumo wa JAZIA Mkoa wa Simiyu, Mfamasia Oscar Tenganamba amesema mfumo huu ulifanyiwa majaribio katika mikoa ya Dodoma, Shinyanga na Morogoro na kuonesha mafanikio makubwa na sasa hivi unatumika katika mikoa yote Tanzania Bara.

Naye mmoja wa wazabuni walioungana na kuwa mshitiri mmoja wa Mkoa katika dawa na Vifaa Tiba (JAZIA) ambaye ni Mkurugenzi wa Operesheni kutoka Kampuni ya Total Health Lab ya jijini Dar es salaam ,  Crispin Mtete amesema kampuni yake na Kampuni ya Mufuruki Traders Company Ltd ya jijini Mwanza zitatoa huduma bora kwa kuzingatia bei elekezi kama mkataba unavyoelekeza.

Mfumo wa JAZIA utatumia mzabuni mmoja aliyechaguliwa kwa ushindani kujazia dawa na vifaa tiba vinavyokosekana katika Bohari ya Dawa (MSD).
 Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini (katikati) akisaini mkataba wa mshitiri mmoja wa Mkoa katika dawa na Vifaa Tiba(JAZIA), Novemba 05, 2018  katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi, waliosimama kushuhudia ni Baadhi ya Wenyeviti wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu.
 Mkurugenzi wa Operesheni kutoka Kampuni ya Total Health Lab ya jijini Dar es salaam ,  Crispin Mtete na Mkurugenzi wa Mufuruki Traders Company Ltd ya jijini Mwanza, Khalifa Mufuruki wakisaii mkataba kama wazabuni walioungana kama mshitiri mmoja wa mkoa wa Simiyu katika kutoa huduma za dawa na vifaa tiba , Novemba 05, 2018 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi.
 Mkurugenzi wa Mufuruki Traders Company Ltd ya jijini Mwanza, Khalifa Mufuruki akizungumza jambo katika uzinduzi rasmi wa mshitiri mmoja wa mkoa katika dawa na vifaa  tiba “ JAZIA” uliofanyika Novemba 05, 2018 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi.
 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, ASF. James John akichangia hoja katika uzinduzi rasmi wa mshitiri mmoja wa mkoa katika dawa na vifaa  tiba “ JAZIA” uliofanyika Novemba 05, 2018 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi.
 Viongozi mbalimbali wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini (hayupo pichani) wakati wa uzinduzi rasmi wa mshitiri mmoja wa mkoa katika dawa na vifaa  tiba “ JAZIA” uliofanyika Novemba 05, 2018 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi.
 Kutoka kulia, Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Anderson Kabuko, Mkurugenzi wa Halmashauri  ya Wilaya ya Bariadi, ASF. James John, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Mariano Mwanyigu, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Bariadi, Melkizedeck Humbe na Katibu Tawala wa Mkoa, Jumanne Sagini  wakisaini mkataba wa mshitiri mmoja wa mkoa katika dawa na vifaa  tiba “ JAZIA”, Novemba 05, 2018 mjini Bariadi.
Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Dkt. Mike Mabimbi akichangia hoja katika uzinduzi rasmi wa mshitiri mmoja wa mkoa katika dawa na vifaa  tiba “ JAZIA” uliofanyika Novemba 05, 2018  katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu Mjini Bariadi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad