HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, October 21, 2018

WAZAZI WAHIMIZA KUUNGA MKONO ELIMU YA KUJITEGEMEA KWA WATOTO WAO

Na Tiganya Vincent
MKUU  wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla amewataka wazazi Mkoani Tabora kutowazuia watoto wao kushiriki katika shughuli mbalimbali za elimu ya kujtegemea kama vile ufugaji na utunzaji wa mifugo ya shughuli na kulima mashamba ya shule yao ili ziweze kuwajengea ujuzi utakaowasaidia baadaye.

Alisema elimu ya kujitegemea inamwezesha mwanafunzi hata kabla au baada ya kumaliza elimu yake ya Msingi kuwa na ujuzi wa kufanya shughuli mbalimbali kitalaamu ikiwemo  kuachana kilimo au ufugaji wa kizamani ambacho hakina tija.

Makalla alitoa kauli hiyowilayani Uyui mkoani Tabora wakati wa ziara ya viongozi wa Mkoa wa Katavi  kujifunza juu ya uendeshaji wa Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP –Tanzania ambao wanatarajia kuanza kuutekeleza katika eneo lao.

Alisema elimu ya kujitegemea itawasaidia watoto kutoa ujuzi walioupata shuleni na kuupeleka ujuzi huo kwa wazazi wao na hivyo kuwa na uzalishaji wa mifugo na mazao ya kilimo kwa tija.

“Mtoto akielimishwa juu ya upandaji kwa kuzingatia vipimo na mistari tangu shule atasaidia kuambukiza elimu hiyo kwa wazazi wake na hivyo kuwa na uzalishaji wa bidhaa nyingi kwa matumizi yao na viwanda vyetu” alisema.

Makalla alisema wazazi wakiona watoto wao wanafundishwa elimu ya kujitegemea kama vile ufugaji , kilimo cha kisasa, wasione kama ni adhabu bali ni faida kubwa wanayopatiwa watoto wao na jamii kwa ujumla.

Aidha Mkuu huyo wa Katavi na ujumbe wake umefurahishwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuinua elimu na kuongeza kipato katika shule mbalimbali mkoani Tabora chini ya Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP –Tanzania.

Alisema kwa kutumia Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP –Tanzania Halmashauri kama ile ya Wilaya ya Tabora -Uyui imefanikiwa kukamilisha ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa katika Shule ya Msingi ILolangulu kwa kiasi cha shilingi milioni 35.

Makallaa alisema hatua hiyo imeonyesha kuwa kwa kuunganisha nguvu pamoja kati ya wananchi,  Kamati ya Shule hiyo na kwa kutumia fedha walizopata kutoka hao wameweza kutekeleza mradi huo  kwa ubora wa hali ya juu.

Makalla alisema mradi huo umetumia nguvu za wananchi ambazo ni milioni 11 na kupata milioni 24 kutoka  Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP –Tanzania wamejenga madarasa matatu ambayo yamefanya kuwepo mazingira mazuri ya watoto kujifunza.

Aliongeza wajifunza kuwa chini ya Mpango huo Mkoa wa Tabora wamefanikiwa kuwasaidia watoto kuweza kujua kusoma, kuandika na kuhesabu kupitia mafunzo ambayo walimu wa elimu ya awali wanapata.

Awali akitoa taarifa ya mradi Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi ILolangulu Mary Zacharia alisema wakazi wa Kijiji cha Ilolangulu waliweza kufanya kazi hiyo baada ya kuunganisha nguvu zao na kuchangishana na kuweza kufikisha jumla ya milioni 11 ambazo ziliwawezesha kufikisha majengo yao katika lenta.

Alisema Serikali baada ya kuona juhudi zao iliwaunga mkono kwa kuwapatia milioni 24 ambazo zimewezesha kuwamalizia kazi zilizokuwa zimebaki na kuwafanikiwa kuwa na madarasa matatu.

Katika hatua nyingine Mwalimu Mkuu huyo alisema Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP –Tanzania uliwapatia  milioni 1.5 kwa ajili ya mradi wa kuongezea kipato Shule ambapo wamefanikiwa kuanzisha mradi wa ufugaji kuku 70.
 Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tabora (Uyui) Said Ntahondi akitoa maelezo kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla (mwenye miwani) juu ya miradi mbalimbali Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP walipotembelea Mkoa wa Tabora kwa ajili ya kujifunza.
 Mkuu wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla (mwenye miwani) alitembelea majengo mbalimbali yaliyokwamilishwa chini ya Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP wakati walipotembelea Mkoa wa Tabora kwa ajili ya kujifunza.
 Mkuu wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla (mwenye miwani) akizungumza na viongozi wa Wilaya ya Uyui mara baada ya kutembelea mradi wa ufugaji kuku  chini ya Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP wakati walipotembelea Mkoa wa Tabora kwa ajili ya kujifunza.
 Mkuu wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla (mwenye miwani) akiwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tabora (Uyui)  Said Ntahondi (kulia) wakiwa kwenye  moja wa madarasa wakati alipoongoza ujumbe kutoka Mkoa wake kuja Tabora kujifunza utekelezaji wa Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP.
 Afisa Taaluma Mkoa wa Tabora (RAO) Silvano Sichone akitoa taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP kwa ujumbe wa Mkoa wa Katavi  walipofika Mkoani humo kwa ajili ya kujifunza mafanikio yaliyotokana na mpango huo.
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Amos Makalla miwani) alizungumza na walimu wa Shule ya Msingi Majengo(hawapo katika picha) wakati alipotembelea Mkoa wa Tabora kujifunza jinsi ya utekelezaji wa   Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania – EQUIP. Picha na Tiganya Vincent

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad