HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 16, 2018

VIPAJI VIPYA KUPAMBA MIAKA 20 YA TWANGAPEPETA, ASHA BARAKA AZUNGUMZIA MAANDALIZI

*Sherehe kufanyika Oktoba 27 ukumbi wa Life Park Dar

Na Khadija Seif, Globu ya jamii
Ni furaha kwa kwenda mbele!Ndivyo unavyoweza kuielezea Bendi ya African Stars Twanga Pepeta ambayo mwaka huu imetimiza miaka 20 tangu kuanzishwa kwake.

Sherehe za kusheherekea miaka ya uwepo wa bendi hiyo iliyosheheni wanamuziki maarufu na wenye vipaji katika muziki was dansi inatarajia kufanyika Oktoba 27 mwaka huu katika ukumbi wa Life Park zamani Mwenge Sinema katika Jiji la Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Kampuni ya African Stars Twangapepeta  mama Asha Baraka amewaaleza leo waandishi wa habari jijini Dar es Salaam namna ambavyo wamejipange kusheherekea miaka 20 tangu kuanzishwa kwa bendi hiyo.

"Katika sherehe hiyo  ya miaka 20 ya bendi yetu  itapambwa  na vipaji vipya kutoka kwa vijana wadogo kama Tarick  na Fetty Kalumba," amesema.

Amefafanua kuwa usiku wa sherehe hiyo kutakua na muda wa kuwaenzi waanzilishi pamoja na wasanii ambao wametangulia mbele ya haki kama Amigo, Abuu Semhando na wengine ambao wamefanya jitihada mpaka hapo bendi ilipofikia.

Asha Baraka ameongeza kwa siku ya kesho kazi zao zitaanza kusambazwa katika vituo vya habari ili kuhamasisha wapenda muziki ,wadau pamoja na viongozi mbalimbali kwa lengo la kuwahamasisha kufika katika sherehe hiyo ya miaka 20 na vibao kama Povu, Rekebisha na vingine vitatumbuizwa kwa mara ya kwanza.

Kwa upande wake Kiongozi Mkuu wa bendi hiyo ambae pia  ni muimbaji wa siku nyingi Luiza Mbutu amewahaidi mashabiki na wadau mbalimbali wa muziki wa dansi kujitokeza kuwaunga mkono kwa hali na mali ili kufanikisha sherehe hizo.

Pia amesema sanjari na hilo  watatembelea kituo cha watoto ya yatima kilichopo  Kinondon Mosco kwa ajili ya kutoa misaada mbalimbali kama kurudisha fadhila kwa jamii pamoja na kuwatembelea  wagonjwa katika Hospitali ya  Mwananyamala iliyopo Kidondoni jijini Dar es Salaam.

Na kwa upande wa waendesha bodaboda watapewa reflecta kwa ajili ya kumuenzi Mwanamuziki Abuu Semhando ambae alipata ajali ya pikipiki.

Wakati huo huo Hassan Mussa 'Super Nyamwela' ambaye ni  Kiongozi wa Watumbuizaji upande wa wanaume wamejipanga katika kuhakikisha wanatoa burudani ya aina yake ambayo itakonga nyoyo za mashabiki,wapenzi na wadau wa bendi hiyo na muziki maarufu nchini.

Amesema umahiri na uhodari wake katika kunengua na kumiliki jukwaa uko palepale au zaidi na kwamba jukwaa la wanenguaji zaidi ya 18 watakuwa jukwaani siku ya sherehe hizo.

Amesema katika idara ya ushereheshaji  kuna baadhi ya wanenguaji wamekua bado wanaiga iga baadhi ya miondoko hivyo wanakaribishwa Kwenye sherehe ya kuzaliwa kwa bendi ya  Twangapepeta  kwani ndio kisima cha burudani.

Msanii mpya ambaye ametambulishwa rasmi kwenye bendi hiyo Fetty Kalumba  amesema amejipanga vizuri kwenye kusherehesha usiku huo na kuhimiza wapenzi wa Twanga kufika na kujumuika pamoja.
 Kiongozi na Muimbaji wa bendi ya Twanga Pepeta Luiza Mbutu akitambulisha baadhi ya vipaji vipya vitakavo tumbuiza usiku wa miaka 20 ya bendi hiyo itakayofanyika katika ukumbi wa Life Park. wa kwanza kulia ni Mkurugenzi wa bendi ya African Stars Asha Baraka.
Mnenguaji wa bendi ya Twanga Pepeta Hassan Musa 'Super Nyamwela'  akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya miaka 20 ya kuanzishwa kwa bendi hiyo itakayofanyika ukumbi wa Life Park Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad