HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, December 15, 2017

WALIODANGANYA RUZUKU YA UCHIMBAJI WATAKIWA KUREJESHA

Serikali imewataka wanufaika wa ruzuku ambao hawakuitumia kama ilivyokusudiwa warejeshe fedha walizopatiwa mara moja na vyombo vya ulinzi na usalama vihakikishe waliohusika kuidhinisha wanawajibishwa. Agizo hilo limetolewa Desemba, 12, 2017 na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo Mkoani Singida wakati wa ziara yake ya kutembelea Migodi ya Dhahabu kwa ajili ya kujionea shughuli zinazoendelea na kuzungumza na wachimbaji.

“Aliyenufaika na ruzuku na hakufanya lolote, arejeshe mara moja fedha hiyo na aliyehusika kuwapatia ruzuku watu hawa hali yakuwa anaelewa hawakuwa na dhamira ya kuendeleza uchimbaji nae achukuliwe hatua,” aliagiza Nyongo.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kushoto aliyenyoosha mkono) akielekeza jambo alipotembelea Mgodi wa Dhahabu wa Mwandami Small Scale Mine uliopo katika Kijiji cha Sambaru, Kata ya Mang’onyi Wilayani Ikungi. 

Agizo hilo linafuatia malalamiko ya wachimbaji wadogo ambao hawakunufaika na mpango huo wa ruzuku ambapo walimueleza kwamba wapo baadhi ya watu wasiostahili lakini walipatiwa ruzuku. Naibu Waziri Nyongo alisema anampongeza Rais John Magufuli kwa uamuzi wake wa kusimamisha utoaji wa ruzuku kwani imeshindwa kufikia matarajio yaliyokusudiwa. Alisema Serikali ilisimamisha utoaji wa ruzuku kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini baada ya kubaini kwamba imeshindwa kuleta mafanikio yaliyokusudiwa.

Nyongo alisema dhamira ya Serikali ya kutoa ruzuku ilikuwa ni kuhakikisha wachimbaji wadogo wa madini nchini wanaweza kuendeleza machimbo yao kwa kufanya shughuli zenye tija kwao na Taifa kwa ujumla. Hata hivyo alisema dhamira hiyo haikuzaa matunda yaliyokuwa yamekusudiwa kwani imedhihirika kwamba ruzuku iliyotolewa haikuwanufaisha walengwa kama ilivyotarajiwa badala yake ilinufaisha watu wachache tofauti na ulivyokuwa mpango mzima wa utoaji wake.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kushoto) akitazama mtambo wa kusaga mawe yenye Madini ya Dhahabu uliopo kwenye Mgodi wa Mzaki na Wenzake uliopo katika Kijiji cha Mwau, Wilayani Ikungi. Kulia ni Mmoja wa Wamiliki wa mgodi huo, Kasirate Mzaki. 

“Wapo wachimbaji wachache ambao walifanikiwa kupata ruzuku na waliweza kuendeleza migodi; japo hawa ni wachache tofauti na malengo ya Serikali,” alisema Naibu Waziri Nyongo. Mbali na hilo, alisema baadhi ya wachimbaji wadogo walipewa ruzuku na walichimba lakini hawakufanikiwa kwani walichimba kwa kubahatisha bila kuwa na elimu ya kutosha ya kutambua uwepo wa mashapo katika maeneo yao.

Kwa kuliona hilo, Nyongo alisema Serikali ipo katika majadiliano na Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini nchini kuona namna ambavyo wanaweza kuwa na uchimbaji wenye tija. Alieleza kwamba Wizara ya Madini kwa kushirikiana na wachimbaji wadogo katika umoja wao wameona ipo haja ya kuwasaidia kufanya utafiti kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ili waweze kutambua maeneo yenye mashapo na hivyo kuepukana na uchimbaji wa kubahatisha.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (katikati) alipotembelea Mgodi wa Dhahabu wa Mwandami Small Scale Mine unaomilikiwa na Yusufu Mwandami (kushoto) uliopo katika Kijiji cha Sambaru, Kata ya Mang’onyi Wilayani Ikungi. 

“Wachimbaji wengi wanafanya uchimbaji kwa kubahatisha na ndiyo maana wapo wengine ambao wanakimbilia kwenye imani za kishirikina. Hii yote ni kukosa elimu, ya utambuzi wa maeneo sahihi,” alisema. Kwa upande wake Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania (FEMATA), John Bina alisema wanaunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha wanakuwa na uchimbaji wenye tija.

Hata hivyo alisema changamoto inayowakabili wachimbaji wadogo walio wengi ni ukosefu wa elimu ya utambuzi wa maeneo sahihi yaliyo na mashapo na kwamba msaada wa Serikali wa kufanya utafiti utawasaidia kufanya uchimbaji wenye faida.
Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania (FEMATA), John Bina (kulia) akizungumza na Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Dhahabu kutoka Wilaya ya Ikungi na Manyoni Mkoani Singida (hawapo pichani), wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa tatu kutoka kushoto) katika Kijiji cha Londoni.
Naibu Waziri wa Madini akizungumza na Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Dhahabu kutoka Wilaya ya Ikungi na Manyoni Mkoani Singida (hawapo pichani), wakati wa ziara yake katika Kijiji cha Londoni.
Baadhi ya Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Dhahabu kutoka Wilaya ya Ikungi na Manyoni Mkoani Singida wakimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani), wakati wa ziara yake katika Kijiji cha Londoni.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad