HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, November 16, 2017

TPDC CUP SASA RASMI SONGO SONGO

Mashindano yajulikanayo kama TPDC Bonanza yenye lengo la kuboresha na kuimarisha afya ya Wakazi wa Songo Songo, ushirikiano pamoja na kujenga vipaji vya michezo kwa vijana wa kike na kiume yanayodhaminiwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) yamezinduliwa rasmi tarehe 13 Novemba, 2017.

Mgeni Rasmi wa Uzinduzi wa Mashindano hayo ambaye ni Meneja Mawasiliano wa TPDC, Marie Msellemu ameeleza kuwa, “Shirika limefarijika sana kufanikiwa kuzindua Mashindano ya Michezo ya Mpira wa Miguu na Pete katika Kijiji cha Songo Songo kwa malengo ya kujenga afya bora kwa kuwa michezo ni nyenzo bora ya kuepuka magonjwa mengi yasiyoambukiza, kuibua vipaji vya michezo, kujenga na kuimarisha uhusiano bora kati ya TPDC na Wananchi.”
Meneja Mawasiliano TPDC akieleza umuhimu wa mashindano ya TPDC CUP katika kuboresha afya na uhusiano bora.

Bi Msellemu amefafanua kuwa, kuwepo kwa Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia na Visima vya Gesi Asilia katika kijiji hicho kunaifanya TPDC kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya jamii ya Kijiji hicho hivyo kwa kuanzishwa kwa mashindano hayo ambayo yatakuwa ya kifanyika kila mwaka ni moja ya sehemu ya utekelezaji wa wajibu wa TPDC kwa Wananchi wa Songo Songo.

Aidha Meneja wa Mawasiliano ameongeza kuwa, “Mashindano haya yataambatana na zoezi la Upimaji Afya ambalo litaanza tarehe 23 hadi 25, Novemba 2017 kwa Wananchi wa Songo Songo ambalo linatarajiwa kujenga uelewa zaidi wa masula ya afya kwa wananchi wa Songo Songo na kuweza kujiepusha na maradhi mbalimbali na hivyo kujenga Jamii imara yenye Afya na Nguvu ambayo itaweza kuendesha Shughuli za Kiuchumi zitakazo jenga na kuimarisha uchumi wa Kijiji na Taifa kwa ujumla.”
Meneja wa Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia cha Songo Songo na Mgeni Rasmi wa Uzinduzi wa Mashindano ya TPDC CUP wakisalimiana na Timu ya Mpira wa Miguu ya Black Rhino kabla ya kuanza kwa mechi yao dhidi ya Heroes.

Awali Meneja wa Kiwanda cha Kuchataka Gesi Asilia ndugu Kondoro Nteminyanda akiwa anamkaribisha Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa mashindano hayo alieleza kuwa uhusiano katika ya Shirika na Jamii ya Wananchi wa Songo Songo ni muhimu kwanza kwasababu wote tunategemeana katika shughuli zetu za kila siku na ili Kiwanda kiweze kifanye kazi yake kwa ufanisi kinahitaji mahusiano bora kati ya Shirika na Wananchi na hivyo shughuli kama hizi za kijamii zinazodhaminiwa na Shirika pamoja manufaa mengine lakini ni muhimu saana katika kujenga na kuendeleza ujirani mwema na ushirikiano wenye tija katika ya Kijiji na Kiwanda.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Songo Songo alieleza kuwa ni furaha ya pekee kwa Kijiji kwa Ushirikiano unaotoka TPDC haswa katika kuanishwa kwa mashindano hayo ya michezo ambayo imeleta hamasa kubwa na furaha kwa wananchi wa Songo Songo.
Mgeni Rasmi akizindua rasmi mashindano ya TPDC CUP katika Uwanja wa Mpira Songo Songo tarehe 13 Novemba, 2017.
“Ndugu zangu wachezaji wa timu zetu pamoja na mashabiki nawaomba tushiriki mashindano haya kwa kufuata Sheria za Uendeshaji wa Michezo za FIFA na Mamlaka nyingine za michezo ili tucheze kwa Amani, furaha na upendo hadi mwisho wa michuano na aliyeshindwa akubali kushindwa ili tumpe hamasa TPDC kuweza kuendelea kudhamini mashindano haya kila mwaka” alifafanua Mwenyekiti wa Kijiji.

Aidha pamoja na kulishukuru Shirika, Mwenyekiti aliomba michezo hiyo pamoja na zoezi la upimaji wa afya liwe la kudumu kama walivyopokea taarifa hapo awali.

Uzinduzi huo ulishuhudia pambano kali lililozikutanisha timu za Black Rhino na Heroes ambapo hadi mwisho wa mchezo timu Black Rhino ilifanikiwa kuitupa nje ya mashindano timu ya Heroes kwa ushindi wa gori moja kwa sifuri.

Katika Mashindano hayo Mshindi wa Kwanza wa Mpira wa Miguu atapata zawadi ya Mbuzi, Jozi moja ya Jezi na Mipira Minne, Mshindi wa Pili atapata Jozi moja ya Jezi na Mipira Miwili na Mshindi wa Tatu atapata Jozi moja ya Jezi na Mpira mmoja.
Kwa upande wa Mpira wa Pete, Mshindi wa Kwanza atapata jozi moja ya Jezi na mipira miwili na Mshindi wa Pili atapata Jezi jozi moja pekee.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad