HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 6, 2016

WANANCHI WA MUSOMA VIJIJINI WAKUMBUKWA NA SERIKALI YA JAJAPAN

Balozi wa Japan nchini Tanzania, Masaharu Yoshida, akiwa ameongozana na mwenyeji wake, Waziri wa Nishati na Madini na Mbunge wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo; akisalimiana na viongozi mbalimbali ngazi ya Mkoa, Wilaya, Vyama vya siasa na viongozi wa Kituo cha Afya cha Murangi, alipowasili katika Kituo hicho hivi karibuni kwa ajili ya hafla ya kutia saini makubaliano ya msaada utakaosaidia upanuzi wa Kituo husika kilichopo wilayani Musoma, Mkoa wa Mara.

Na Veronica Simba - Musoma

Serikali ya Japan kupitia kwa Balozi wake nchini, Masaharu Yoshida, imetia saini makubaliano ya shilingi za Tanzania milioni 170  kwa ajili ya kusaidia mradi wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Murangi kilichopo wilayani Musoma, Mkoa wa Mara. 

Makubaliano hayo yaliyosainiwa baina ya Balozi huyo na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Flora Rajabu Yongolo, kituoni hapo hivi karibuni, yameshuhudiwa na Waziri wa Nishati na Madini ambaye pia ni Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo. 

Wengine walioshiriki hafla hiyo na kushuhudia tukio hilo la utiaji saini, ni viongozi mbalimbali ngazi ya Mkoa, Wilaya na Halmashauri pamoja na wananchi wa Jimbo husika.
Balozi wa Japan nchini Tanzania, Masaharu Yoshida (kulia) na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Flora Rajabu Yongolo, wakisaini hati za makubaliano ya msaada wa shilingi za Tanzania milioni 170 uliotolewa na Serikali ya Japan kusaidia Mradi wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Murangi kilichopo wilayani Musoma, mkoani Mara. Wanaoshuhudia (waliosimama) ni Waziri wa Nishati na Madini na Mbunge wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Annarose Nyamubi.
Akizungumza mara baada ya kutia saini, Balozi Yoshida alisema kuwa, Serikali ya Japan imeamua kutoa msaada huo kutokana na uhaba wa vifaa tiba na zana katika Kituo hicho cha Afya, ambavyo havitoshelezi ongezeko la idadi na mahitaji ya wagonjwa.

Akifafanua zaidi, Balozi Yoshida alisema kuwa, msaada huo utatumika kujenga nyumba za wafanyakazi, choo cha wagonjwa, shimo la kutupia kondo la nyuma na kurekebisha tanuru la kuchomea taka za hospitalini kwa lengo la kuwapatia wagonjwa huduma safi na salama pamoja na kuboresha mandhari ya kazi kwa wauguzi. 

Waziri wa Nishati na Madini ambaye pia ni Mbunge wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo (aliyeshika kipaza sauti), akimshukuru na kumuaga Balozi wa Japani nchini Tanzania, mara baada ya kuhitimisha hafla ya kutia saini makubaliano ya msaada utakaosaidia upanuzi wa kituo cha afya cha Murangi kilichopo wilayani Musoma, Mkoa wa Mara. 
Aidha, Balozi Yoshida alisema kuwa, Serikali ya Japan inaihakikishia Serikali ya Tanzania kuwa, itaendelea kutoa michango yake katika kuisaidia Tanzania kupitia mpango huo.
Kwa upande wake, Prof Muhongo amewataka wananchi wa Jimbo hilo kuendelea kuchapa kazi kwa bidii zaidi na ubunifu na kuwahakikishia kuwa maendeleo zaidi yanakuja jimboni humo.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Annarose Nyamubi, akizungumza katika hafla hiyo. 

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Flora Rajabu Yongolo, alimshukuru Balozi wa Japan kwa msaada ambao Serikali yake imeutoa na kumhakikishia kuwa rasilimali zote za mradi husika zitatunzwa na kutumika ipasavyo.

Kituo cha cha Murangi kilijengwa mwaka 1972. Ni Kituo kikubwa cha Afya wilayani Musoma na hupokea wagonjwa wengi wa rufaa kutoka Zahanati Nane (8) wilayani humo.

Mkataba uliosainiwa ni kupitia mfuko wa mpango wa Miradi midogomidogo kwa ajili ya usalama wa binadamu yaani Grant Assistance for Grassroots Human Security Projects (GGHSP).
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Flora Rajab Yongolo, akitoa neno la shukrani kwa Serikali ya Japan kwa msaada uliotolewa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad